[1] Mwimbieni BWANA wimbo mpya, kwa maana ametenda mambo ya ajabu; kitanga chake cha kuume na mkono wake mtakatifu umemfanyia wokovu. [2] BWANA ameufanya wokovu wake ujulikane na amedhihirisha haki yake kwa mataifa. [3] Ameukumbuka upendo wake na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli; miisho yote ya dunia imeuona wokovu wa Mungu wetu. [4] Mpigieni BWANA kelele za shangwe, dunia yote, ipaze sauti kwa nyimbo za shangwe na vinanda; [5] mwimbieni BWANA kwa kinubi, kwa kinubi na sauti za kuimba, [6] kwa tarumbeta na mvumo wa baragumu za pembe za kondoo dume: shangilieni kwa furaha mbele za BWANA, aliye Mfalme. [7] Bahari na ivume na kila kiliomo ndani yake, dunia na wote wakaao ndani yake. [8] Mito na ipige makofi, milima na iimbe pamoja kwa furaha, [9] vyote na viimbe mbele za BWANA, kwa maana yuaja kuhukumu dunia. Atahukumu dunia kwa haki na mataifa kwa haki.