[1] Mwimbieni BWANA wimbo mpya; mwimbieni BWANA dunia yote. [2] Mwimbieni BWANA, lisifuni jina lake; tangazeni wokovu wake siku baada ya siku. [3] Tangazeni utukufu wake katikati ya mataifa, matendo yake ya ajabu miongoni mwa mataifa yote. [4] Kwa kuwa BWANA ni mkuu mwenye kustahili kusifiwa kuliko wote; yeye ni wa kuogopwa kuliko miungu yote. [5] Kwa maana miungu yote ya mataifa ni sanamu, lakini BWANA aliziumba mbingu. [6] Fahari na enzi viko mbele yake; nguvu na utukufu vimo patakatifu pake. [7] Mpeni BWANA, enyi jamaa za mataifa, mpeni BWANA utukufu na nguvu. [8] Mpeni BWANA utukufu unaostahili jina lake; leteni sadaka na mje katika nyua zake. [9] Mwabuduni BWANA katika uzuri wa utakatifu wake; dunia yote na itetemeke mbele zake. [10] Katikati ya mataifa semeni, “BWANA anatawala.” Ulimwengu ameuweka imara, hauwezi kusogezwa; atawahukumu watu kwa uadilifu. [11] Mbingu na zishangilie, nchi na ifurahi; bahari na ivume, na vyote vilivyomo ndani yake; [12] mashamba na yashangilie, pamoja na vyote vilivyomo ndani yake. Kisha miti yote ya msituni itaimba kwa furaha; [13] itaimba mbele za BWANA kwa maana anakuja, anakuja kuihukumu dunia. Ataihukumu dunia kwa haki, na mataifa katika kweli yake.