[1] Yeye akaaye mahali pa salama pake Yeye Aliye Juu Sana, atadumu katika uvuli wake Mwenyezi. [2] Nitasema kumhusu BWANA, “Yeye ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye ninamtumaini.” [3] Hakika yeye ataniokoa na mtego wa mwindaji, na maradhi ya kuambukiza ya kuua. [4] Atakufunika kwa manyoya yake, chini ya mbawa zake utapata kimbilio, uaminifu wake utakuwa ngao na kinga yako. [5] Hutaogopa vitisho vya usiku, wala mshale urukao mchana, [6] wala maradhi ya kuambukiza yanayonyemelea gizani, wala tauni iharibuyo adhuhuri. [7] Ijapo watu elfu wataangukia kando yako, kumi elfu mkono wako wa kuume, lakini haitakukaribia wewe. [8] Utatazama tu kwa macho yako na kuona adhabu ya waovu. [9] Kama ukimfanya Aliye Juu Sana kuwa makao yako: naam, BWANA ambaye ni kimbilio langu, [10] basi hakuna madhara yatakayokupata wewe, hakuna maafa yataikaribia hema yako. [11] Kwa kuwa atawaagiza malaika zake kwa ajili yako, wakulinde katika njia zako zote. [12] Mikononi mwao watakuinua, ili usijikwae mguu wako kwenye jiwe. [13] Utawakanyaga simba na nyoka wakali, simba mkubwa na nyoka utawaponda kwa miguu. [14] BWANA asema, “Kwa kuwa ananipenda, nitamwokoa; nitamlinda, kwa kuwa analikiri Jina langu. [15] Ataniita, nami nitamjibu; nitakuwa pamoja naye katika taabu, nitamwokoa na kumheshimu. [16] Kwa siku nyingi nitamshibisha na kumwonyesha wokovu wangu.”