[1] Ni vyema kumshukuru BWANA na kuliimbia jina lako, Ee Uliye Juu Sana, [2] kuutangaza upendo wako asubuhi, na uaminifu wako wakati wa usiku, [3] kwa zeze yenye nyuzi kumi na kwa sauti ya kinubi. [4] Ee BWANA, kwa kuwa matendo yako yamenifurahisha, nitaziimba kwa shangwe kazi za mikono yako. [5] Ee BWANA, tazama jinsi yalivyo makuu matendo yako, tazama jinsi yalivyo ya kina mawazo yako! [6] Mjinga hafahamu, mpumbavu haelewi, [7] ingawa waovu huchipua kama majani na wote watendao mabaya wanastawi, wataangamizwa milele. [8] Bali wewe, Ee BWANA, utatukuzwa milele. [9] Ee BWANA, hakika adui zako, hakika adui zako wataangamia. Wote watendao mabaya watatawanyika. [10] Umeitukuza pembe yangu kama ile ya nyati dume, mafuta mazuri yamemiminwa juu yangu. [11] Macho yangu yamewaona adui zangu wakishindwa, masikio yangu yamesikia maangamizi ya adui zangu waovu. [12] Wenye haki watastawi kama mtende, watakuwa kama mwerezi wa Lebanoni, [13] waliopandwa katika nyumba ya BWANA, watastawi katika nyua za Mungu wetu. [14] Wakati wa uzee watakuwa bado wanazaa matunda, watakuwa wabichi tena wamejaa nguvu, [15] wakitangaza, “BWANA ni mkamilifu; yeye ni Mwamba wangu, na ndani yake hamna uovu.”