[1] BWANA, wewe umekuwa makao yetu katika vizazi vyote. [2] Kabla ya kuzaliwa milima au hujaumba dunia na ulimwengu, wewe ni Mungu tangu milele hata milele. [3] Huwarudisha watu mavumbini, ukisema, “Rudini mavumbini, enyi wanadamu.” [4] Kwa maana kwako miaka elfu ni kama siku moja iliyokwisha pita, au kama kesha la usiku. [5] Unawatowesha wanadamu katika usingizi wa kifo, nao ni kama majani machanga ya asubuhi: [6] ingawa asubuhi yanachipua, ifikapo jioni huwa yamenyauka na kukauka. [7] Tumeangamizwa kwa hasira yako na tumetishwa kwa ghadhabu yako. [8] Umeyaweka maovu yetu mbele yako, dhambi zetu za siri katika nuru ya uwepo wako. [9] Tumeishi siku zetu zote chini ya ghadhabu yako, tunamaliza miaka yetu kwa kuomboleza. [10] Siku zetu za kuishi ni miaka sabini, au miaka themanini ikiwa tuna nguvu, lakini yote ni ya shida na taabu, nazo zapita haraka, nasi twatoweka. [11] Ni nani ajuaye nguvu za hasira yako? Kwa maana ghadhabu yako ni kubwa kama hofu tunayopaswa kuwa nayo kwako. [12] Tufundishe kuzihesabu siku zetu vizuri, ili tujipatie moyo wa hekima. [13] Ee BWANA, uwe na huruma! Utakawia hata lini? Wahurumie watumishi wako. [14] Tushibishe asubuhi kwa upendo wako usiokoma, ili tuweze kuimba kwa shangwe na kufurahi siku zetu zote. [15] Utufurahishe kulingana na siku ulizotuadhibu, kulingana na miaka tuliyotaabika. [16] Matendo yako na yaonekane kwa watumishi wako, utukufu wako kwa watoto wao. [17] Wema wa BWANA Mungu wetu uwe juu yetu; uzithibitishe kazi za mikono yetu: naam, uzithibitishe kazi za mikono yetu.