Zaburi 89:1-52 ONEN
[1] Nitaimba juu ya upendo mkuu wa BWANA milele; kwa kinywa changu nitajulisha uaminifu wako ujulikane kwa vizazi vyote. [2] Nitatangaza kuwa upendo wako unasimama imara milele na uaminifu wako umeuthibitisha mbinguni. [3] Ulisema, “Nimefanya agano na mteule wangu, nimemwapia mtumishi wangu Daudi, [4] ‘Nitaimarisha uzao wako milele na kudumisha ufalme wako kwa vizazi vyote.’ ” [5] Ee BWANA, mbingu zinayasifu maajabu yako, uaminifu wako pia katika kusanyiko la watakatifu. [6] Kwa kuwa ni nani katika mbingu anayeweza kulinganishwa na BWANA? Ni nani miongoni mwa viumbe vya mbinguni aliye kama BWANA? [7] Katika kusanyiko la watakatifu, Mungu huogopwa sana, anahofiwa kuliko wote wanaomzunguka. [8] Ee BWANA Mwenye Nguvu Zote, ni nani aliye kama wewe? Ee BWANA, wewe ni mwenye nguvu, na uaminifu wako unakuzunguka. [9] Wewe unatawala bahari yenye msukosuko; wakati mawimbi yake yanapoinuka, wewe unayatuliza. [10] Wewe ulimponda Rahabu kama mmojawapo wa waliochinjwa; kwa mkono wako wenye nguvu, uliwatawanya adui zako. [11] Mbingu ni zako, nayo nchi pia ni yako, uliuwekea ulimwengu msingi pamoja na vyote vilivyomo. [12] Uliumba kaskazini na kusini; Tabori na Hermoni wanaliimbia jina lako kwa furaha. [13] Mkono wako umejaa uwezo; mkono wako una nguvu, mkono wako wa kuume umetukuzwa. [14] Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chako cha enzi; upendo na uaminifu vinakutangulia. [15] Heri ni wale ambao wamejifunza kukusifu kwa shangwe, wanaotembea katika mwanga wa uwepo wako, Ee BWANA. [16] Wanashangilia katika jina lako mchana kutwa, wanafurahi katika haki yako. [17] Kwa kuwa wewe ni utukufu na nguvu yao, kwa wema wako unatukuza pembe yetu. [18] Naam, ngao yetu ni mali ya BWANA, na mfalme wetu mali ya Aliye Mtakatifu wa Israeli. [19] Ulizungumza wakati fulani katika maono, kwa watu wako waaminifu, ukasema: “Nimeweka nguvu kwa shujaa, nimemwinua kijana miongoni mwa watu. [20] Nimemwona Daudi, mtumishi wangu, na nimemtia mafuta yangu matakatifu. [21] Kitanga changu kitamtegemeza, hakika mkono wangu utamtia nguvu. [22] Hakuna adui atakayemtoza ushuru, hakuna mtu mwovu atakayemwonea. [23] Nitawaponda adui zake mbele zake na kuwaangamiza watesi wake. [24] Upendo wangu mkamilifu utakuwa pamoja naye, kwa Jina langu pembe yake itatukuzwa. [25] Nitauweka mkono wake juu ya bahari, mkono wake wa kuume juu ya mito. [26] Naye ataniita kwa sauti, ‘Wewe ni Baba yangu, Mungu wangu, Mwamba na Mwokozi wangu.’ [27] Nitamteua pia awe mzaliwa wangu wa kwanza, aliyetukuka kuliko wafalme wote wa dunia. [28] Nitadumisha upendo wangu kwake milele, na agano langu naye litakuwa imara. [29] Nitaudumisha uzao wake milele, kiti chake cha enzi kama mbingu zinavyodumu. [30] “Kama wanae wataacha amri yangu na wasifuate sheria zangu, [31] kama wakihalifu maagizo yangu na kutoshika amri zangu, [32] nitaadhibu dhambi yao kwa fimbo, uovu wao kwa kuwapiga, [33] lakini sitauondoa upendo wangu kwake, wala sitausaliti uaminifu wangu kamwe. [34] Mimi sitavunja agano langu wala sitabadili lile ambalo midomo yangu imelitamka. [35] Mara moja na kwa milele, nimeapa kwa utakatifu wangu, nami sitamdanganya Daudi: [36] kwamba uzao wake utaendelea milele, na kiti chake cha enzi kitadumu mbele zangu kama jua; [37] kitaimarishwa milele kama mwezi, shahidi mwaminifu angani.” [38] Lakini wewe umemkataa, umemdharau, umemkasirikia sana mpakwa mafuta wako. [39] Umelikana agano lako na mtumishi wako, na umeinajisi taji yake mavumbini. [40] Umebomoa kuta zake zote, na ngome zake zote umezifanya kuwa magofu. [41] Wote wapitao karibu wamemnyangʼanya mali zake; amekuwa dharau kwa jirani zake. [42] Umeutukuza mkono wa kuume wa adui zake, umewafanya watesi wake wote washangilie. [43] Umegeuza makali ya upanga wake, na hukumpa msaada katika vita. [44] Umeikomesha fahari yake, na kukiangusha kiti chake cha enzi. [45] Umezifupisha siku za ujana wake, umemfunika kwa vazi la aibu. [46] Hata lini, Ee BWANA? Utajificha milele? Ghadhabu yako itawaka kama moto hata lini? [47] Kumbuka jinsi maisha yangu yanavyopita haraka. Ni kwa ubatili kiasi gani umemuumba mwanadamu! [48] Ni mtu gani awezaye kuishi na asione kifo, au kujiokoa mwenyewe kutoka nguvu za kaburi? [49] Ee BWANA, uko wapi upendo wako mkuu wa mwanzoni, ambao katika uaminifu wako ulimwapia Daudi? [50] Bwana kumbuka jinsi mtumishi wako amesimangwa, jinsi ninavyovumilia moyoni mwangu dhihaka za mataifa yote, [51] dhihaka ambazo kwazo adui zako wamenisimanga, Ee BWANA, ambazo kwazo wamesimanga kila hatua ya mpakwa mafuta wako. [52] Msifuni BWANA milele! Amen na Amen.
