[1] Ee BWANA, Mungu uniokoaye, nimelia mbele zako usiku na mchana. [2] Maombi yangu yafike mbele zako, utegee kilio changu sikio lako. [3] Kwa maana nafsi yangu imejaa taabu, na maisha yangu yanakaribia kaburi. [4] Nimehesabiwa miongoni mwa wale waendao shimoni, niko kama mtu asiye na nguvu. [5] Nimetengwa pamoja na wafu, kama waliochinjwa walalao kaburini, ambao huwakumbuki tena, ambao wamekatiliwa mbali na uangalizi wako. [6] Umenitupa katika shimo lenye kina kirefu sana, katika vina vya giza nene. [7] Ghadhabu yako imekuwa nzito juu yangu, umenigharikisha kwa mawimbi yako yote. [8] Umenitenga na rafiki zangu wa karibu na kunifanya chukizo kwao. Nimezuiliwa, wala siwezi kutoroka; [9] nuru ya macho yangu imefifia kwa ajili ya huzuni. Ee BWANA, ninakuita kila siku, ninakunyooshea wewe mikono yangu. [10] Je, wewe huwaonyesha wafu maajabu yako? Je, wale waliokufa huinuka na kukusifu? [11] Je, upendo wako hutangazwa kaburini, uaminifu wako katika Uharibifu? [12] Je, maajabu yako hujulikana mahali pa giza, au matendo yako ya haki katika nchi ya usahaulifu? [13] Lakini ninakulilia wewe, Ee BWANA, unisaidie; asubuhi maombi yangu huja mbele zako. [14] Ee BWANA, kwa nini unanikataa na kunificha uso wako? [15] Tangu ujana wangu nimeteseka, nikakaribia kifo; nimepatwa na hofu zako, nami nimekata tamaa. [16] Ghadhabu yako imepita juu yangu; hofu zako zimeniangamiza. [17] Mchana kutwa zinanizunguka kama mafuriko; zimenimeza kabisa. [18] Umeniondolea marafiki na wapendwa wangu; giza limekuwa ndilo rafiki yangu wa karibu kuliko wote.