[1] Ee BWANA, ulionyesha wema kwa nchi yako. Ulimrejeshea Yakobo baraka zake. [2] Ulisamehe uovu wa watu wako, na kufunika dhambi zao zote. [3] Uliweka kando ghadhabu yako yote na umegeuka na kuiacha hasira yako kali. [4] Ee Mungu Mwokozi wetu, uturejeshe tena, nawe uiondoe chuki yako juu yetu. [5] Je, utatukasirikia milele? Utaendeleza hasira yako kwa vizazi vyote? [6] Je, hutatuhuisha tena, ili watu wako wakufurahie? [7] Utuonyeshe upendo wako usiokoma, Ee BWANA, utupe wokovu wako. [8] Nitasikiliza lile atakalosema Mungu aliye BWANA; anaahidi amani kwa watu wake, watakatifu wake: lakini nao wasirudie upumbavu. [9] Hakika wokovu wake uko karibu na wale wamchao, ili utukufu wake udumu katika nchi yetu. [10] Upendo na uaminifu hukutana pamoja, haki na amani hubusiana. [11] Uaminifu huchipua kutoka nchi, haki hutazama chini kutoka mbinguni. [12] Naam, hakika BWANA atatoa kilicho chema, nayo nchi yetu itazaa mavuno yake. [13] Haki itatangulia mbele yake na kutengeneza njia kwa ajili ya hatua zake.