[1] Ee BWANA Mwenye Nguvu Zote, makao yako yapendeza kama nini! [2] Nafsi yangu inatamani sana, naam, hata kuona shauku, kwa ajili ya nyua za BWANA; moyo wangu na mwili wangu vinamlilia Mungu Aliye Hai. [3] Hata shomoro amejipatia makao, mbayuwayu amejipatia kiota mahali awezapo kuweka makinda yake: mahali karibu na madhabahu yako, Ee BWANA Mwenye Nguvu Zote, Mfalme wangu na Mungu wangu. [4] Heri wale wanaokaa nyumbani mwako, wanaokusifu wewe daima. [5] Heri wale ambao nguvu zao ziko kwako, na njia ziendazo Sayuni zimo mioyoni mwao. [6] Wanapopita katika Bonde la Baka, hulifanya mahali pa chemchemi, pia mvua za vuli hulijaza kwa madimbwi. [7] Huendelea toka nguvu hadi nguvu, hadi kila mmoja afikapo mbele za Mungu huko Sayuni. [8] Ee BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote, sikia maombi yangu; nisikilize, Ee Mungu wa Yakobo. [9] Ee Mungu, uitazame ngao yetu, mtazame kwa wema mpakwa mafuta wako. [10] Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu mahali pengine; afadhali ningekuwa bawabu katika nyumba ya Mungu wangu kuliko kukaa katika mahema ya waovu. [11] Kwa kuwa BWANA ni jua na ngao, BWANA hutoa wema na heshima; hakuna kitu chema anachowanyima wale ambao hawana hatia. [12] Ee BWANA Mwenye Nguvu Zote, heri ni mtu yule anayekutumaini wewe.