[1] Ee BWANA, sikia na unijibu, kwa maana mimi ni maskini na mhitaji. [2] Linda maisha yangu, kwa maana nimejiweka kwako, wewe ni Mungu wangu, mwokoe mtumishi wako anayekutumaini. [3] Ee BWANA, nihurumie mimi, kwa maana ninakuita mchana kutwa. [4] Mpe mtumishi wako furaha, kwa kuwa kwako wewe, Ee BWANA, ninainua nafsi yangu. [5] Ee BWANA, wewe ni mwema na mwenye kusamehe, umejaa upendo kwa wote wakuitao. [6] Ee BWANA, sikia maombi yangu, sikiliza kilio changu unihurumie. [7] Katika siku ya shida yangu nitakuita, kwa maana wewe utanijibu. [8] Ee BWANA, katikati ya miungu hakuna kama wewe, hakuna matendo ya kulinganishwa na yako. [9] Ee BWANA, mataifa yote uliyoyafanya yatakuja na kuabudu mbele zako; wataliletea utukufu jina lako. [10] Kwa maana wewe ni mkuu, na unafanya mambo ya ajabu; wewe peke yako ndiwe Mungu. [11] Ee BWANA, nifundishe njia yako, nami nitakwenda katika kweli yako; nipe moyo usiositasita, ili niweze kulicha jina lako. [12] Ee BWANA wangu, nitakusifu kwa moyo wote; nitaliadhimisha jina lako milele. [13] Kwa maana upendo wako ni mkuu kwangu; umeniokoa kutoka kwenye vilindi vya kaburi. [14] Ee Mungu, wenye majivuno wananishambulia; kundi la watu wakatili linatafuta uhai wangu: watu wasiokuheshimu wewe. [15] Lakini wewe, Ee BWANA, ni Mungu wa huruma na neema, si mwepesi wa hasira, bali ni mwingi wa upendo na uaminifu. [16] Nigeukie na unihurumie; mpe mtumishi wako nguvu zako, mwokoe mwana wa mtumishi wako wa kike. [17] Nipe ishara ya wema wako, ili adui zangu waione nao waaibishwe, kwa kuwa wewe, Ee BWANA, umenisaidia na kunifariji.