[1] Ee Mungu, usinyamaze kimya, usinyamaze, Ee Mungu, usitulie. [2] Tazama watesi wako wanafanya fujo, jinsi adui zako wanavyoinua vichwa vyao. [3] Kwa hila, wanafanya shauri dhidi ya watu wako, wanafanya shauri baya dhidi ya wale unaowapenda. [4] Wanasema, “Njooni, tuwaangamize kama taifa, ili jina la Israeli lisikumbukwe tena.” [5] Kwa nia moja wanapanga mashauri mabaya pamoja, wanafanya muungano dhidi yako, [6] mahema ya Edomu na Waishmaeli, ya Wamoabu na Wahagari, [7] Gebali, Amoni na Amaleki, Ufilisti, pamoja na watu wa Tiro. [8] Hata Ashuru wameungana nao kuwapa nguvu wazao wa Loti. [9] Uwatendee kama vile ulivyowatendea Midiani, na kama vile ulivyowatendea Sisera na Yabini hapo kijito cha Kishoni, [10] ambao waliangamia huko Endori na wakawa kama takataka juu ya nchi. [11] Wafanye wakuu wao kama Orebu na Zeebu, watawala wao kama Zeba na Salmuna, [12] ambao walisema, “Na tumiliki nchi ya malisho ya Mungu.” [13] Ee Mungu wangu, wapeperushe kama mavumbi ya kisulisuli, kama makapi yapeperushwayo na upepo. [14] Kama vile moto uteketezavyo msitu au mwali wa moto unavyounguza milima, [15] wafuatilie kwa tufani yako na kuwafadhaisha kwa dhoruba yako. [16] Funika nyuso zao kwa aibu ili watu walitafute jina lako, Ee BWANA. [17] Wao na waaibishwe na kufadhaishwa milele, na waangamie kwa aibu. [18] Hebu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni BWANA, kwamba wewe peke yako ndiwe Uliye Juu Sana ya dunia yote.