[1] Nilimlilia Mungu ili anisaidie, nilimlilia Mungu ili anisikie. [2] Nilipokuwa katika taabu, nilimtafuta Bwana, usiku nilinyoosha mikono bila kuchoka na nafsi yangu ilikataa kufarijika. [3] Ee Mungu, nilikukumbuka wewe, nikalia kwa huzuni; nikatafakari, roho yangu ikadhoofika. [4] Ulizuia macho yangu kufumba; nilikuwa nasumbuka, nikashindwa kusema. [5] Nilitafakari juu ya siku zilizopita, miaka mingi iliyopita, [6] nilikumbuka nilivyoimba nyimbo usiku. Moyo wangu ulitafakari na roho yangu ikauliza: [7] “Je, Bwana atakataa milele? Je, hatatenda mema tena? [8] Je, upendo wake usio na mwisho umetoweka milele? Je, ahadi yake imekoma nyakati zote? [9] Je, Mungu amesahau kuwa na huruma? Je, katika hasira amezuia huruma yake?” [10] Ndipo nikawaza, “Huu ndio udhaifu wangu: lakini nitakumbuka miaka ya mkono wa kuume wa Aliye Juu Sana.” [11] Nitayakumbuka matendo ya BWANA; naam, nitaikumbuka miujiza yako ya zamani. [12] Nitazitafakari kazi zako zote na kuyawaza matendo yako makuu. [13] Ee Mungu, njia zako ni takatifu. Ni mungu yupi aliye mkuu kama Mungu wetu? [14] Wewe ndiwe Mungu utendaye miujiza, umeonyesha uwezo wako katikati ya mataifa. [15] Kwa mkono wako wenye nguvu umewakomboa watu wako, uzao wa Yakobo na Yosefu. [16] Maji yalikuona, Ee Mungu, maji yalikuona yakakimbia, vilindi vilitetemeka. [17] Mawingu yalimwaga maji, mbingu zikatoa ngurumo kwa radi, mishale yako ikametameta huku na huko. [18] Ngurumo yako ilisikika katika upepo wa kisulisuli, umeme wako wa radi ukaangaza dunia, nchi ikatetemeka na kutikisika. [19] Njia yako ilipita baharini, mapito yako kwenye maji makuu, ingawa nyayo zako hazikuonekana. [20] Uliongoza watu wako kama kundi kwa mkono wa Mose na Aroni.