Zaburi 78:1-72 ONEN
[1] Enyi watu wangu, sikieni mafundisho yangu, sikilizeni maneno ya kinywa changu. [2] Nitafungua kinywa changu kwa mafumbo, nitazungumza mambo yaliyofichika, mambo ya kale: [3] yale ambayo tuliyasikia na kuyajua, yale ambayo baba zetu walituambia. [4] Hatutayaficha kwa watoto wao; tutakiambia kizazi kijacho matendo yastahiliyo sifa ya BWANA, uweza wake, na maajabu aliyoyafanya. [5] Aliagiza amri kwa Yakobo na akaweka sheria katika Israeli, ambazo aliwaamuru baba zetu wawafundishe watoto wao, [6] ili kizazi kijacho kizijue, pamoja na watoto ambao watazaliwa, nao pia wapate kuwaeleza watoto wao. [7] Ndipo wangeweka tumaini lao kwa Mungu, nao wasingesahau matendo yake, bali wangalizishika amri zake. [8] Ili wasifanane na baba zao, waliokuwa kizazi cha ukaidi na uasi, ambao roho zao hazikuwa na uaminifu kwake, ambao roho zao hazikumwamini. [9] Watu wa Efraimu, ingawa walijifunga pinde, walikimbia siku ya vita. [10] Hawakulishika agano la Mungu na walikataa kuishi kwa sheria yake. [11] Walisahau aliyokuwa ameyatenda, maajabu aliyokuwa amewaonyesha. [12] Alitenda miujiza machoni mwa baba zao, huko Soani, katika nchi ya Misri. [13] Aliigawanya bahari akawapitisha, alifanya maji yasimame imara kama ukuta. [14] Aliwaongoza kwa wingu mchana na kwa nuru kutoka kwenye moto usiku kucha. [15] Alipasua miamba jangwani na akawapa maji tele kama bahari, [16] alitoa vijito kutoka kwenye jabali lililochongoka, akayafanya maji yatiririke kama mito. [17] Lakini waliendelea kutenda dhambi dhidi yake, wakiasi jangwani dhidi ya Aliye Juu Sana. [18] Kwa makusudi walimjaribu Mungu, wakidai vyakula walivyovitamani. [19] Walinena dhidi ya Mungu, wakisema, “Je, Mungu aweza kuandaa meza jangwani? [20] Alipopiga mwamba, maji yalitoka kwa nguvu, vijito vikatiririka maji mengi. Lakini je, aweza kutupa chakula pia? Je, anaweza kuwapa watu wake nyama?” [21] BWANA alipowasikia, alikasirika sana, moto wake ukawa dhidi ya Yakobo, na ghadhabu yake ikawaka dhidi ya Israeli, [22] kwa kuwa hawakumwamini Mungu, wala kuutumainia ukombozi wake. [23] Hata hivyo alitoa amri kwa anga zilizo juu na kufungua milango ya mbingu, [24] akawanyeshea mana ili watu wale; aliwapa nafaka ya mbinguni. [25] Watu walikula mkate wa malaika, akawatumia chakula chote ambacho wangeliweza kula. [26] Aliachia upepo wa mashariki kutoka kwenye mbingu na kuuongoza upepo wa kusini kwa uwezo wake. [27] Aliwanyeshea nyama kama mavumbi, ndege warukao kama mchanga wa pwani. [28] Aliwafanya washuke ndani ya kambi yao, kuzunguka mahema yao yote. [29] Walikula na kusaza, kwa maana alikuwa amewapa kile walichotamani. [30] Kabla hawajamaliza kula walichokitamani, hata kilipokuwa kingali bado vinywani mwao, [31] hasira ya Mungu ikawaka juu yao, akawaua wale waliokuwa na nguvu zaidi miongoni mwao, akiwaangusha vijana wa Israeli. [32] Licha ya haya yote, waliendelea kutenda dhambi, licha ya maajabu yake, hawakuamini. [33] Kwa hiyo akamaliza siku zao katika ubatili na miaka yao katika vitisho. [34] Kila mara Mungu alipowaua baadhi yao, waliosalia walimtafuta, walimgeukia tena kwa shauku. [35] Walikumbuka kwamba Mungu alikuwa Mwamba wao, kwamba Mungu Aliye Juu Sana alikuwa Mkombozi wao. [36] Lakini walimdanganya kwa vinywa vyao, wakisema uongo kwa ndimi zao, [37] mioyo yao haikuwa thabiti kwake, wala hawakuwa waaminifu katika agano lake. [38] Hata hivyo alikuwa na huruma, alisamehe maovu yao na hakuwaangamiza. Mara kwa mara alizuia hasira yake, wala hakuchochea ghadhabu yake yote. [39] Alikumbuka kwamba wao walikuwa nyama tu, upepo upitao ambao haurudi. [40] Mara ngapi walimwasi jangwani na kumhuzunisha nyikani! [41] Walimjaribu Mungu mara kwa mara, wakamkasirisha yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli. [42] Hawakukumbuka uwezo wake, siku aliyowakomboa kutoka kwa mtesi, [43] siku aliyoonyesha ishara zake za ajabu huko Misri, maajabu yake huko Soani. [44] Aligeuza mito yao kuwa damu, hawakuweza kunywa maji kutoka vijito vyao. [45] Aliwapelekea makundi ya mainzi yakawala, na vyura wakawaharibu. [46] Aliruhusu tunutu kuharibu mimea yao, mazao yao kwa nzige. [47] Aliharibu mizabibu yao kwa mvua ya mawe na mikuyu yao kwa mvua iliyochangamana na theluji. [48] Aliwaachia mifugo yao mvua ya mawe, akayapiga makundi ya wanyama wao kwa radi. [49] Aliwafungulia hasira yake kali, ghadhabu yake, hasira na uadui, na kundi la malaika wa kuharibu. [50] Aliitengenezea njia hasira yake, hakuwaepusha na kifo, bali aliwaachia tauni. [51] Aliwapiga wazaliwa wote wa kwanza wa Misri, matunda ya kwanza ya ujana katika mahema ya Hamu. [52] Lakini aliwatoa watu wake kama kundi, akawaongoza kama kondoo kupitia jangwani. [53] Aliwaongoza salama, wala hawakuogopa, bali bahari iliwameza adui zao. [54] Hivyo akawaleta hadi kwenye mpaka wa nchi yake takatifu, hadi nchi ya vilima ambayo mkono wake wa kuume ulikuwa umeitwaa. [55] Aliyafukuza mataifa mbele yao, na kuwagawia nchi zao kama urithi, aliwakalisha makabila ya Israeli katika makao yao. [56] Lakini wao walimjaribu Mungu, na kuasi dhidi ya Yeye Aliye Juu Sana, wala hawakuzishika sheria zake. [57] Kama baba zao, hawakuwa thabiti wala waaminifu, wakawa wasioweza kutegemewa kama upinde wenye kasoro. [58] Wakamkasirisha Mungu kwa mahali pao pa juu pa kuabudia miungu, wakachochea wivu wake kwa sanamu zao. [59] Wakati Mungu alipowasikia, alikasirika sana, akamkataa Israeli kabisa. [60] Akaiacha hema ya Shilo, hema aliyokuwa ameiweka katikati ya wanadamu. [61] Akalipeleka Sanduku la nguvu zake utumwani, utukufu wake mikononi mwa adui. [62] Aliachia watu wake wauawe kwa upanga, akaukasirikia sana urithi wake. [63] Moto uliwaangamiza vijana wao, na wanawali wao hawakuimbiwa nyimbo za arusi, [64] makuhani wao waliuawa kwa upanga, wala wajane wao hawakuweza kulia. [65] Ndipo Bwana alipoamka kama vile kuamka usingizini, kama vile mtu aamkavyo kutoka kwenye bumbuazi la mvinyo. [66] Aliwapiga na kuwashinda adui zake, akawatia katika aibu ya milele. [67] Ndipo alipozikataa hema za Yosefu, hakulichagua kabila la Efraimu, [68] lakini alilichagua kabila la Yuda, Mlima Sayuni, ambao aliupenda. [69] Alijenga patakatifu pake kama vilele, kama dunia ambayo aliimarisha milele. [70] Akamchagua Daudi mtumishi wake na kumtoa kwenye mazizi ya kondoo. [71] Kutoka kuchunga kondoo alimleta kuwa mchungaji wa watu wake Yakobo, wa Israeli urithi wake. [72] Naye Daudi aliwachunga kwa uadilifu wa moyo, kwa mikono ya ustadi aliwaongoza.
