[1] Ee Mungu, mbona umetukataa milele? Mbona hasira yako inatoka moshi juu ya kondoo wa malisho yako? [2] Kumbuka watu uliowanunua zamani, kabila la urithi wako, ambao uliwakomboa: Mlima Sayuni, ambamo uliishi. [3] Geuza hatua zako kuelekea magofu haya ya kudumu, uharibifu wote huu ambao adui ameuleta pale patakatifu. [4] Adui zako wamenguruma pale ulipokutana nasi, wanaweka bendera zao kama alama. [5] Walifanya kama watu wanaotumia mashoka kukata kichaka cha miti. [6] Walivunjavunja milango yote iliyonakshiwa kwa mashoka na vishoka vyao. [7] Waliteketeza kabisa mahali pako patakatifu, wakayanajisi makao ya Jina lako. [8] Walisema mioyoni mwao, “Tutawaponda kabisa!” Walichoma kila mahali ambapo Mungu aliabudiwa katika nchi. [9] Hatukupewa ishara za miujiza; hakuna manabii waliobaki, hakuna yeyote kati yetu ajuaye hali hii itachukua muda gani. [10] Ee Mungu, mtesi atakudhihaki mpaka lini? Je, adui watalitukana jina lako milele? [11] Kwa nini unazuia mkono wako, mkono wako wa kuume? Uutoe kutoka makunjo ya vazi lako na uwaangamize! [12] Lakini wewe, Ee Mungu, ni mfalme wangu tangu zamani, unaleta wokovu duniani. [13] Ni wewe uliyeigawanya bahari kwa uweza wako; ulivunja vichwa vya wanyama wakubwa wa kutisha katika maji. [14] Ni wewe uliyeponda vichwa vya Lewiathani nawe ukamtoa kama chakula kwa viumbe vya jangwani. [15] Ni wewe uliyefungua chemchemi na vijito, ulikausha mito ambayo ilikuwa ikitiririka daima. [16] Mchana ni wako, nao usiku ni wako pia, uliziweka jua na mwezi. [17] Ni wewe uliyeiweka mipaka yote ya dunia, ulifanya kiangazi na masika. [18] Ee BWANA, kumbuka jinsi mtesi alivyokudhihaki, jinsi watu wapumbavu walivyolitukana jina lako. [19] Usiukabidhi uhai wa njiwa wako kwa wanyama wakali wa mwitu; usisahau kabisa uhai wa watu wako wanaoteseka milele. [20] Likumbuke agano lako, maana mara kwa mara mambo ya jeuri yamejaa katika sehemu za giza nchini. [21] Usiruhusu walioonewa warudi nyuma kwa aibu; maskini na wahitaji hebu walisifu jina lako. [22] Inuka, Ee Mungu, ujitetee; kumbuka jinsi wapumbavu wanavyokudhihaki mchana kutwa. [23] Usipuuze makelele ya watesi wako, ghasia za adui zako, zinazoinuka mfululizo.