[1] Hakika Mungu ni mwema kwa Israeli, kwa wale ambao mioyo yao ni safi. [2] Bali kwangu mimi, miguu yangu ilikuwa karibu kuteleza; nilikuwa karibu mguu wangu kuachia uliposimama. [3] Kwa maana niliwaonea wivu wenye kujivuna nilipoona kufanikiwa kwa waovu. [4] Wao hawana taabu, miili yao ina afya na nguvu. [5] Hawapati shida zinazowataabisha watu wengine, wala hawapati mapigo kama wanadamu wengine. [6] Kwa hiyo kiburi ni mkufu wao, wamejivika jeuri. [7] Uovu hutoka katika mioyo yao iliyokufa ganzi, majivuno maovu kutoka mioyoni mwao hauna kikomo. [8] Hudhihaki na kusema kwa ukorofi, katika majivuno yao wanatishia kutesa. [9] Vinywa vyao huweka madai hata kwa mbingu, nazo ndimi zao humiliki duniani. [10] Kwa hiyo watu wao huwageukia na kunywa maji tele. [11] Wanasema, “Mungu awezaje kujua? Je, Yeye Aliye Juu Sana anayo maarifa?” [12] Hivi ndivyo walivyo waovu: siku zote hawajali, wanaongezeka katika utajiri. [13] Hakika nimeuweka moyo wangu safi bure, ni bure nimenawa mikono yangu nisiwe na hatia. [14] Mchana kutwa nimetaabika, nimeadhibiwa kila asubuhi. [15] Kama ningesema, “Nitasema hivi,” ningelikuwa nimewasaliti watoto wako. [16] Nilipojaribu kuelewa haya yote, yalikuwa magumu kwangu kuelewa. [17] Mpaka nilipoingia patakatifu pa Mungu, ndipo nilipotambua mwisho wao. [18] Hakika unawaweka mahali pa utelezi, unawaangusha chini kwa uharibifu. [19] Tazama jinsi wanavyoangamizwa ghafula, wanatoweshwa kabisa na vitisho! [20] Kama ndoto mtu aamkapo, hivyo wakati uinukapo, Ee BWANA, utawatowesha kama ndoto. [21] Wakati moyo wangu ulipohuzunishwa, na roho yangu ilipotiwa uchungu, [22] nilikuwa mpumbavu na mjinga, nilikuwa mnyama mkatili mbele yako. [23] Hata hivyo niko pamoja nawe siku zote, umenishika mkono wangu wa kuume. [24] Unaniongoza kwa shauri lako, hatimaye utaniingiza katika utukufu. [25] Nani niliye naye mbinguni ila wewe? Dunia haina chochote ninachokitamani ila wewe. [26] Mwili na moyo wangu vyaweza kushindwa, bali Mungu ni nguvu ya moyo wangu na fungu langu milele. [27] Wale walio mbali nawe wataangamia, unawaangamiza wote wasio waaminifu kwako. [28] Lakini kwangu mimi, ni vyema kuwa karibu na Mungu. Nimemfanya BWANA Mwenyezi kimbilio langu; nami nitayasimulia matendo yako yote.