[1] Ee Mungu, mjalie mfalme aamue kwa haki yako, mwana wa mfalme kwa haki yako. [2] Atawaamua watu wako kwa haki, watu wako walioonewa kwa haki. [3] Milima italeta mafanikio kwa watu, vilima tunda la haki. [4] Atawatetea walioonewa miongoni mwa watu na atawaokoa watoto wa wahitaji, ataponda mdhalimu. [5] Atadumu kama jua lidumuvyo, kama mwezi, vizazi vyote. [6] Atakuwa kama mvua inyeshayo juu ya shamba lililofyekwa, kama manyunyu yanyeshayo ardhi. [7] Katika siku zake wenye haki watastawi; mafanikio yatakuwepo mpaka mwezi utakapokoma. [8] Atatawala kutoka bahari hadi bahari na kutoka Mto mpaka miisho ya dunia. [9] Makabila ya jangwani watamsujudia, na adui zake wataramba mavumbi. [10] Wafalme wa Tarshishi na wa pwani za mbali watamletea kodi; wafalme wa Sheba na Seba watampa zawadi. [11] Wafalme wote watamsujudia na mataifa yote yatamtumikia. [12] Kwa maana atamwokoa mhitaji anayemlilia, aliyeonewa asiye na wa kumsaidia. [13] Atawahurumia wanyonge na wahitaji na kuwaokoa wahitaji kutoka mauti. [14] Atawaokoa kutoka uonevu na ukatili, kwani damu yao ni ya thamani machoni pake. [15] Aishi maisha marefu! Na apewe dhahabu ya Sheba. Watu wamwombee daima na kumbariki mchana kutwa. [16] Nafaka ijae tele katika nchi yote, juu ya vilele vya vilima na istawi. Tunda lake na listawi kama Lebanoni, listawi kama majani ya kondeni. [17] Jina lake na lidumu milele, na lidumu kama jua. Mataifa yote yatabarikiwa kupitia kwake, nao watamwita aliyebarikiwa. [18] BWANA Mungu, Mungu wa Israeli, apewe sifa, yeye ambaye peke yake hutenda mambo ya ajabu. [19] Jina lake tukufu lisifiwe milele, ulimwengu wote ujae utukufu wake. Amen na Amen. [20] Huu ndio mwisho wa maombi ya Daudi mwana wa Yese.