Zaburi 71:1-24 ONEN
[1] Ee BWANA, nimekukimbilia wewe, usiache nikaaibika kamwe. [2] Kwa haki yako uniponye na kuniokoa, unitegee sikio lako uniokoe. [3] Uwe kwangu mwamba wa kimbilio, mahali nitakapokimbilia kila wakati; toa amri ya kuniokoa, kwa kuwa wewe ni mwamba wangu na ngome yangu. [4] Ee Mungu wangu uniokoe kutoka kwenye mkono wa mwovu, kutoka kwenye makucha ya watu wabaya na wakatili. [5] Kwa kuwa umekuwa tumaini langu, Ee BWANA Mwenyezi, tegemeo langu tangu ujana wangu. [6] Tangu kuzaliwa nimekutegemea wewe, ulinitoa tumboni mwa mama yangu. Nitakusifu wewe daima. [7] Nimekuwa kama kioja kwa wengi, lakini wewe ni kimbilio langu imara. [8] Kinywa changu kimejazwa sifa zako, nikitangaza utukufu wako mchana kutwa. [9] Usinitupe wakati wa uzee, wala usiniache nguvu zangu zinapopungua. [10] Kwa maana adui zangu wananisengenya, wale wanaonivizia kuniua wafanya hila. [11] Wanasema, “Mungu amemwacha, mkimbilieni mkamkamate, kwani hakuna wa kumwokoa.” [12] Ee Mungu, usiwe mbali nami, njoo haraka kunisaidia, Ee Mungu wangu. [13] Washtaki wangu na waangamie kwa aibu, wale wanaotaka kunidhuru na wafunikwe kwa dharau na fedheha. [14] Lakini mimi, nitatumaini siku zote, nitakusifu zaidi na zaidi. [15] Kinywa changu kitasimulia haki yako, wokovu wako mchana kutwa, ingawa sifahamu kipimo chake. [16] Ee BWANA Mwenyezi, nitakuja na kutangaza matendo yako makuu, nitatangaza haki yako, yako peke yako. [17] Ee Mungu, umenifundisha tangu ujana wangu, hadi leo ninatangaza matendo yako ya ajabu. [18] Ee Mungu, usiniache, hata niwapo mzee wa mvi, mpaka nitangaze uwezo wako kwa kizazi kijacho, nguvu zako kwa wote watakaokuja baadaye. [19] Ee Mungu, haki yako imefika juu katika mbingu, wewe ambaye umefanya mambo makuu. Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe? [20] Ingawa umenifanya nipate taabu, nyingi na chungu, utanihuisha tena, kutoka vilindi vya dunia utaniinua tena. [21] Utaongeza heshima yangu na kunifariji tena. [22] Ee Mungu wangu, nitakusifu kwa kinubi kwa ajili ya uaminifu wako; Ee Uliye Mtakatifu wa Israeli, nitakuimbia sifa kwa zeze. [23] Midomo yangu itapaza sauti kwa furaha ninapokuimbia sifa, mimi, ambaye umenikomboa. [24] Ulimi wangu utasimulia matendo yako ya haki mchana kutwa, kwa maana wale waliotaka kunidhuru, wameaibishwa na kufadhaishwa.
