Zaburi 69:1-36 ONEN
[1] Ee Mungu, niokoe, kwa maana maji yamenifika shingoni. [2] Ninazama kwenye vilindi vya matope, pasipo mahali pa kukanyaga, Nimefika kwenye maji makuu, mafuriko yamenigharikisha. [3] Nimechoka kwa kuomba msaada, koo langu limekauka. Macho yangu yanafifia, nikimtafuta Mungu wangu. [4] Wale wanaonichukia bila sababu ni wengi kuliko nywele za kichwa changu; wengi ni adui kwangu bila sababu, wale wanaotafuta kuniangamiza. Ninalazimishwa kurudisha kitu ambacho sikuiba. [5] Ee Mungu, wewe unajua upumbavu wangu, wala hatia yangu haikufichika kwako. [6] Ee Bwana, ewe BWANA Mwenye Nguvu Zote, wakutumainio wasiaibishwe kwa ajili yangu; wakutafutao wasifedheheshwe kwa ajili yangu, Ee Mungu wa Israeli. [7] Kwa maana nimestahimili dharau kwa ajili yako, aibu imefunika uso wangu. [8] Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, mgeni kwa wana wa mama yangu mwenyewe. [9] Kwa kuwa wivu wa nyumba yako unanila, matukano ya wale wanaokutukana yameniangukia. [10] Ninapolia na kufunga, lazima nivumilie matusi. [11] Ninapovaa nguo ya gunia, watu hunidharau. [12] Wale wanaoketi mlangoni wananisimanga, nimekuwa wimbo wa walevi. [13] Lakini Ee BWANA, ninakuomba, kwa wakati ukupendezao; katika upendo wako mkuu, Ee Mungu, unijibu kwa wokovu wako wa hakika. [14] Uniokoe katika matope, usiniache nizame; niokoe na hao wanichukiao, kutoka kwenye vilindi vya maji. [15] Usiache mafuriko yanigharikishe au vilindi vinimeze, au shimo lifumbe kinywa chake juu yangu. [16] Ee BWANA, unijibu, kwa wema wa upendo wako; kwa huruma zako nyingi unigeukie. [17] Usimfiche mtumishi wako uso wako, uharakishe kunijibu, kwa sababu niko katika shida. [18] Njoo karibu uniokoe, nikomboe kwa sababu ya adui zangu. [19] Unajua jinsi ninavyodharauliwa, kufedheheshwa na kuaibishwa, adui zangu wote unawajua. [20] Dharau zimenivunja moyo na nimekata tamaa, nimetafuta wa kunihurumia, lakini sikumpata, wa kunituliza, lakini sikumpata. [21] Waliweka nyongo katika chakula changu na walinipa siki nilipokuwa na kiu. [22] Meza iliyoandaliwa mbele yao na iwe mtego, nayo iwe upatilizo na tanzi. [23] Macho yao yatiwe giza ili wasiweze kuona, nayo migongo yao iinamishwe daima. [24] Uwamwagie ghadhabu yako, hasira yako kali na iwapate. [25] Mahali pao na pawe ukiwa, wala asiwepo yeyote atakayeishi katika mahema yao. [26] Kwa kuwa wanawatesa wale uliowajeruhi, na kuzungumza juu ya maumivu ya wale uliowaumiza. [27] Walipize uovu juu ya uovu, usiwaache washiriki katika wokovu wako. [28] Wafutwe kutoka kitabu cha uzima na wasiorodheshwe pamoja na wenye haki. [29] Mimi niko katika maumivu na dhiki; Ee Mungu, wokovu wako na unihifadhi. [30] Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo, nami nitamtukuza kwa kumtolea shukrani. [31] Hili litampendeza BWANA kuliko ngʼombe dume, zaidi ya fahali akiwa na pembe na kwato zake. [32] Maskini wataona na kufurahi: ninyi mnaomtafuta Mungu, mioyo yenu na iishi! [33] BWANA huwasikia wahitaji wala hadharau watu wake waliotekwa. [34] Mbingu na dunia zimsifu, bahari na vyote viendavyo ndani yake, [35] kwa maana Mungu ataiokoa Sayuni na kuijenga tena miji ya Yuda. Kisha watu watafanya makao yao humo na kuimiliki, [36] watoto wa watumishi wake watairithi na wale wote walipendao jina lake wataishi humo.
