Zaburi 68:1-35 ONEN
[1] Mungu na ainuke, watesi wake watawanyike, adui zake na wakimbie mbele zake. [2] Kama vile moshi upeperushwavyo na upepo, vivyo hivyo uwapeperushe mbali, kama vile nta iyeyukavyo kwenye moto, vivyo hivyo waovu na waangamie mbele za Mungu. [3] Bali wenye haki na wafurahi, washangilie mbele za Mungu, wafurahi na kushangilia. [4] Mwimbieni Mungu, liimbieni sifa jina lake, mtukuzeni yeye aendeshwaye juu ya mawingu: jina lake ni BWANA, furahini mbele zake. [5] Baba wa yatima, mtetezi wa wajane, ni Mungu katika makao yake matakatifu. [6] Mungu huwaweka wapweke katika jamaa, huwaongoza wafungwa wakiimba, bali waasi huishi katika nchi kame. [7] Ee Mungu, ulipowatangulia watu wako, ulipopita nyikani, [8] dunia ilitikisika, mbingu zikanyesha mvua, mbele za Mungu, Yule wa Sinai, mbele za Mungu, Mungu wa Israeli. [9] Ee Mungu, ulinyesha mvua nyingi na kuiburudisha ardhi iliyokuwa imechoka. [10] Ee Mungu, watu wako waliishi huko, nawe kwa wingi wa utajiri wako uliwapa maskini mahitaji yao. [11] Bwana alitangaza neno, waliolitangaza neno hilo walikuwa kundi kubwa: [12] “Wafalme na majeshi walikimbia upesi, watu waliobaki kambini waligawana nyara. [13] Hata ulalapo katikati ya mioto ya kambini, mabawa ya njiwa wangu yamefunikwa kwa fedha, manyoya yake kwa dhahabu ingʼaayo.” [14] Wakati Mwenyezi alipowatawanya wafalme katika nchi, ilikuwa kama theluji iliyoanguka juu ya Salmoni. [15] Milima ya Bashani ni milima iliyotukuka, milima ya Bashani ina vilele vilivyochongoka. [16] Enyi milima yenye vilele vilivyochongoka, kwa nini mnakazia macho kwa wivu, katika mlima Mungu anaochagua kutawala, ambako BWANA mwenyewe ataishi milele? [17] Magari ya Mungu ni makumi ya maelfu, na maelfu ya maelfu; Bwana amekuja kutoka Sinai hadi katika patakatifu pake. [18] Ulipopanda juu, uliteka mateka, ukapokea vipawa kutoka kwa wanadamu, hata kutoka kwa wale walioasi, ili wewe, Ee BWANA Mungu, upate kuishi huko. [19] Sifa apewe Bwana, Mungu Mwokozi wetu, ambaye siku kwa siku hutuchukulia mizigo yetu. [20] Mungu wetu ni Mungu aokoaye, BWANA Mwenyezi hutuokoa na kifo. [21] Hakika Mungu ataponda vichwa vya adui zake, vichwa vya hao waendao katika njia za dhambi. [22] Bwana alisema, “Nitawarudisha kutoka Bashani; nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari, [23] ili uweze kuchovya miguu yako katika damu ya adui zako, huku ndimi za mbwa wako zikiwa na fungu lake.” [24] Ee Mungu, maandamano yako yameonekana, maandamano ya Mungu wangu, Mfalme wangu, yakielekea patakatifu pake. [25] Mbele wako waimbaji, baada yao wapiga vinanda, pamoja nao wako wanawali wakipiga matari. [26] Msifuni Mungu katika kusanyiko kubwa, msifuni BWANA katika kusanyiko la Israeli. [27] Liko kabila dogo la Benyamini likiwaongoza, wakifuatwa na kundi kubwa la watawala wa Yuda, hatimaye watawala wa Zabuloni na Naftali. [28] Ee Mungu, amuru uwezo wako, Ee Mungu tuonyeshe nguvu zako, kama ulivyofanya hapo awali. [29] Kwa sababu ya Hekalu lako Yerusalemu wafalme watakuletea zawadi. [30] Mkemee mnyama aliyeko kwenye manyasi, kundi la mafahali katikati ya ndama za mataifa. Na walete minara ya madini ya fedha wakinyenyekea. Tawanya mataifa yapendayo vita. [31] Wajumbe watakuja kutoka Misri, Kushi atajisalimisha kwa Mungu. [32] Mwimbieni Mungu, enyi falme za dunia, mwimbieni Bwana sifa, [33] mwimbieni sifa yeye apandaye mbingu za kale zilizo juu, yeye angurumaye kwa sauti kuu. [34] Tangazeni uwezo wa Mungu, ambaye fahari yake iko juu ya Israeli, ambaye uwezo wake uko katika anga. [35] Ee Mungu, wewe unatisha katika mahali patakatifu pako, Mungu wa Israeli huwapa watu wake uwezo na nguvu. Mungu Asifiwe!
