[1] Ee Mungu, sifa zakungojea katika Sayuni; kwako wewe nadhiri zetu zitatimizwa. [2] Ewe usikiaye maombi, kwako wewe watu wote watakuja. [3] Tulipokuwa tumefunikwa kabisa na dhambi, wewe ulisamehe makosa yetu. [4] Heri wale uliowachagua na kuwaleta karibu ili waishi katika nyua zako! Tunashibishwa kwa mema ya nyumba yako, mema ya Hekalu lako takatifu. [5] Unatujibu kwa matendo ya kushangaza ya haki, Ee Mungu Mwokozi wetu, tumaini la miisho yote ya duniani na la bahari zilizo mbali sana, [6] uliyeumba milima kwa uwezo wako, ukiwa umejivika nguvu, [7] uliyenyamazisha dhoruba za bahari, ngurumo za mawimbi yake, na ghasia za mataifa. [8] Wale wanaoishi mbali sana wanaogopa maajabu yako, kule asubuhi ipambazukiapo na kule jioni inakofifilia umeziita nyimbo za furaha. [9] Waitunza nchi na kuinyeshea, waitajirisha kwa wingi. Vijito vya Mungu vimejaa maji ili kuwapa watu nafaka, kwa maana wewe umeviamuru. [10] Umeilowesha mifereji yake na kusawazisha kingo zake; umeilainisha kwa manyunyu na kuibariki mimea yake. [11] Umeuvika mwaka taji ya baraka, magari yako yanafurika kwa wingi. [12] Mbuga za majani za jangwani umezineemesha; vilima vimevikwa furaha. [13] Penye nyanda za malisho pamejaa makundi ya wanyama, na mabonde yamepambwa kwa mavuno; vyote vinashangilia kwa furaha na kuimba.