[1] Mpigieni Mungu kelele za shangwe, dunia yote! [2] Imbeni utukufu wa jina lake; mpeni sifa zake kwa utukufu! [3] Mwambieni Mungu, “Jinsi gani yalivyo ya kutisha matendo yako! Uwezo wako ni mkuu mno kiasi kwamba adui wananyenyekea mbele zako. [4] Dunia yote yakusujudia, wanakuimbia wewe sifa, wanaliimbia sifa jina lako.” [5] Njooni mwone yale Mungu aliyoyatenda, mambo ya kutisha aliyoyatenda miongoni mwa wanadamu! [6] Alifanya bahari kuwa nchi kavu, wakapita kati ya maji kwa miguu, njooni, tumshangilie. [7] Yeye hutawala kwa uwezo wake milele, macho yake huangalia mataifa yote: waasi wasithubutu kujiinua dhidi yake. [8] Enyi mataifa, msifuni Mungu wetu, sauti ya sifa yake isikike, [9] ameyahifadhi maisha yetu na kuizuia miguu yetu kuteleza. [10] Ee Mungu, wewe ulitujaribu, ukatusafisha kama fedha. [11] Umetuingiza kwenye nyavu na umetubebesha mizigo mizito migongoni mwetu. [12] Uliwaruhusu watu watukalie vichwani, tulipita kwenye moto na kwenye maji, lakini ulituleta kwenye nchi iliyojaa utajiri tele. [13] Nitakuja hekaluni mwako na sadaka za kuteketezwa na kukutimizia nadhiri zangu: [14] nadhiri ambazo midomo yangu iliahidi na nilizotamka kwa kinywa changu nilipokuwa katika shida. [15] Nitakutolea dhabihu za wanyama wanono na sadaka za kondoo dume, nitakutolea mafahali na mbuzi. [16] Njooni msikilize ninyi nyote mnaomcha Mungu, nami niwaambie aliyonitendea. [17] Nilimlilia kwa kinywa changu, sifa zake zilikuwa katika ulimi wangu. [18] Kama ningekuwa nimeyaficha maovu moyoni mwangu, Bwana asingekuwa amenisikiliza; [19] lakini hakika Mungu amenisikiliza na amesikia sauti yangu katika maombi. [20] Sifa apewe Mungu, ambaye hakulikataa ombi langu wala kunizuilia upendo wake!