[1] Ee Mungu, uniokoe na adui zangu, unilinde kutokana na hao wanaoinuka dhidi yangu. [2] Uniponye na watu watendao mabaya, uniokoe kutokana na wamwagao damu. [3] Tazama wanavyonivizia! Watu wakali wananifanyia hila, ingawa Ee BWANA, mimi sijakosea wala kutenda dhambi. [4] Sijatenda kosa; hata hivyo wako tayari kunishambulia. Inuka unisaidie, uone hali yangu mbaya! [5] Ee BWANA Mwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli! Zinduka uyaadhibu mataifa yote, usionyeshe huruma kwa wasaliti. [6] Hurudi wakati wa jioni, wakibweka kama mbwa, wakiuzurura mji. [7] Tazama yale wanayotema kutoka vinywa vyao, hutema upanga kutoka midomo yao, nao husema, “Ni nani atakayetusikia?” [8] Lakini wewe, BWANA, uwacheke; unayadharau mataifa hayo yote. [9] Ee nguvu yangu, ninakutazama wewe, wewe, Ee Mungu, ndiwe ngome yangu, [10] Mungu wangu unipendaye. Mungu atanitangulia, naye atanifanya niwachekelee wale wanaonisingizia. [11] Lakini usiwaue, Ee BWANA, ngao yetu, au sivyo watu wangu watasahau. Katika uwezo wako wafanye watangetange na uwashushe chini. [12] Kwa ajili ya dhambi za vinywa vyao, kwa ajili ya maneno ya midomo yao, waache wanaswe katika kiburi chao. Kwa ajili ya laana na uongo wanaotamka, [13] wateketeze katika ghadhabu, wateketeze hadi wasiwepo tena. Ndipo itakapofahamika katika miisho ya dunia kwamba Mungu anatawala juu ya Yakobo. [14] Hurudi jioni, wakibweka kama mbwa, wakiuzurura mji. [15] Wanatangatanga wakitafuta chakula, wasipotosheka hubweka kama mbwa. [16] Lakini mimi nitaziimba nguvu zako, asubuhi nitaimba juu ya upendo wako; kwa maana wewe ndiwe ngome yangu na kimbilio langu wakati wa shida. [17] Ee uliye Nguvu zangu, ninakuimbia sifa. Wewe, Ee Mungu, ndiwe ngome yangu, Mungu unipendaye.