[1] Enyi watawala, je, kweli mwanena kwa haki? Je, mnahukumu kwa unyofu miongoni mwa watu? [2] La, mioyoni mwenu mnatunga udhalimu, na mikono yenu hupima jeuri duniani. [3] Waovu ni wapotovu tangu kuzaliwa kwao, toka tumboni mwa mama zao ni wakaidi na husema uongo. [4] Sumu yao ni kama sumu ya nyoka, kama ile ya fira ambaye ameziba masikio yake, [5] ambaye hatasikia sauti ya kutumbuiza ya mwaguzi, hata kama mganga angecheza kwa ustadi kiasi gani. [6] Ee Mungu, yavunje meno katika vinywa vyao; Ee BWANA, vunja meno makali ya hao simba! [7] Na watoweke kama maji yapitayo kwa kasi, wavutapo pinde zao, mishale yao na iwe butu. [8] Kama konokono ayeyukavyo akitembea, kama mtoto aliyezaliwa akiwa mfu, wasilione jua. [9] Kabla vyungu vyenu havijapata moto wa kuni za miiba, zikiwa mbichi au kavu, waovu watakuwa wamefagiliwa mbali. [10] Wenye haki watafurahi waonapo wakilipizwa kisasi, watakapochovya nyayo zao katika damu ya waovu. [11] Ndipo wanadamu watasema, “Hakika utulivu wa wenye haki bado una thawabu, hakika kuna Mungu ahukumuye dunia.”