[1] Ee Mungu, umetukataa na kutokea ghafula juu yetu, umekasirika: sasa turejeshe upya! [2] Umetetemesha nchi na kuipasua; uiponye mavunjiko yake, kwa maana inatetemeka. [3] Umewaonyesha watu wako nyakati za kukata tamaa; umetunywesha mvinyo unaotuyumbisha. [4] Kwa wale wanaokucha wewe, umewainulia bendera, ili iweze kutwekwa dhidi ya upinde. [5] Tuokoe na utusaidie kwa mkono wako wa kuume, ili wale uwapendao wapate kuokolewa. [6] Mungu amenena kutoka patakatifu pake: “Nitaigawa Shekemu kwa ushindi na kulipima Bonde la Sukothi. [7] Gileadi ni yangu na Manase ni yangu; Efraimu ni kofia yangu ya chuma, nayo Yuda ni fimbo yangu ya utawala. [8] Moabu ni sinia langu la kunawia, juu ya Edomu natupa kiatu changu; nashangilia kwa kushindwa kwa Ufilisti.” [9] Ni nani atakayenipeleka hadi mji wenye ngome? Ni nani atakayeniongoza hadi nifike Edomu? [10] Ee Mungu, si ni wewe uliyetukataa sisi, na hutoki tena na majeshi yetu? [11] Tuletee msaada dhidi ya adui, kwa maana msaada wa mwanadamu haufai kitu. [12] Kwa msaada wa Mungu tutapata ushindi, naye atawaponda adui zetu.