[1] Unihurumie, Ee Mungu, unihurumie, kwa maana nafsi yangu inakukimbilia. Chini ya uvuli wa mbawa zako nitakimbilia mpaka maafa yapite. [2] Namlilia Mungu Aliye Juu Sana, Mungu atimizaye makusudi yake kwangu. [3] Hutumana kutoka mbinguni na kuniokoa, akiwakemea wale wanaonifuatilia vikali; Mungu huutuma upendo wake na uaminifu wake. [4] Niko katikati ya simba, nimelala katikati ya wanyama wenye njaa kuu: watu ambao meno yao ni mikuki na mishale, ambao ndimi zao ni panga kali. [5] Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, utukufu wako na uenee duniani kote. [6] Waliitegea miguu yangu nyavu, nikainamishwa chini na dhiki. Wamechimba shimo katika njia yangu, lakini wametumbukia humo wao wenyewe. [7] Ee Mungu, moyo wangu ni thabiti; nitaimba na kusifu kwa moyo wangu wote. [8] Amka, nafsi yangu! Amka, kinubi na zeze! Nitayaamsha mapambazuko. [9] Nitakusifu wewe, Ee BWANA, katikati ya mataifa; nitaimba habari zako, katikati ya jamaa za watu. [10] Kwa maana upendo wako ni mkuu, waenea hadi mbinguni, uaminifu wako unazifikia anga. [11] Ee Mungu, utukuzwe juu mbinguni, utukufu wako na uwe duniani pote.