[1] Ee Mungu unihurumie, maana watu wananifuatia vikali; mchana kutwa wanazidisha mashambulizi yao. [2] Wasingiziaji wangu wananifuatia mchana kutwa, wengi wananishambulia kwa kiburi chao. [3] Wakati ninapoogopa, nitakutumaini wewe. [4] Katika Mungu, ambaye neno lake ninalisifu, katika Mungu ninatumaini; sitaogopa. Mwanadamu apatikanaye na kufa, atanitenda nini? [5] Mchana kutwa wanayageuza maneno yangu, siku zote wanapanga shauri la kunidhuru. [6] Wananifanyia hila, wanajificha, wanatazama hatua zangu, wakiwa na shauku ya kuutoa uhai wangu. [7] Wasiepuke kwa vyovyote, Ee Mungu, katika hasira yako yaangushe mataifa. [8] Andika maombolezo yangu, orodhesha machozi yangu katika gombo lako: je, haya hayapo katika kumbukumbu zako? [9] Ndipo adui zangu watarudi nyuma ninapoita msaada. Kwa hili nitajua kwamba Mungu yuko upande wangu. [10] Katika Mungu, ambaye neno lake ninalisifu, katika BWANA, ambaye neno lake ninalisifu, [11] katika Mungu ninatumaini, sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini? [12] Ee Mungu, nina nadhiri kwako, nitakutolea wewe sadaka zangu za shukrani. [13] Kwa kuwa umeniokoa toka kwenye mauti na miguu yangu kwenye kujikwaa, ili niweze kuenenda mbele za Mungu katika nuru ya uzima.