[1] Ee Mungu, sikiliza maombi yangu, wala usidharau hoja yangu. [2] Nisikie na unijibu. Mawazo yangu yananisumbua na nimehangaishwa [3] kwa sauti ya adui, kwa kukaziwa macho na waovu, kwa sababu wananiletea mateso juu yangu na kunitukana kwa hasira zao. [4] Moyo wangu umejaa uchungu, hofu ya kifo imenishambulia. [5] Woga na kutetemeka vimenizunguka, hofu kuu imenigharikisha. [6] Nilisema, “Laiti ningekuwa na mbawa za njiwa! Ningeruka niende mbali kupumzika. [7] Ningalitorokea mbali sana na kukaa jangwani, [8] ningaliharakisha kwenda mahali pa salama, mbali na tufani kali na dhoruba.” [9] Ee BWANA, uwatahayarishe waovu na uwachanganyishie semi zao, maana nimeona jeuri na ugomvi mjini. [10] Usiku na mchana wanazunguka juu ya kuta zake, uovu na dhuluma vimo ndani yake. [11] Nguvu za uharibifu zinatenda kazi mjini, vitisho na uongo haviondoki mitaani mwake. [12] Kama aliyenitukana ni adui yangu, ningevumilia, kama mtu mwovu angejiinua dhidi yangu, ningejificha asinione. [13] Kumbe ni wewe, mwenzangu, mshiriki na rafiki yangu wa karibu, [14] ambaye awali tulifurahia ushirika mzuri, tulipokuwa tukienda na umati hekaluni mwa Mungu. [15] Kifo na kiwajie adui zangu ghafula, na washuke kuzimu wangali hai, kwa maana uovu upo ndani yao. [16] Lakini ninamwita Mungu, naye BWANA huniokoa. [17] Jioni, asubuhi na adhuhuri ninalia kwa huzuni, naye husikia sauti yangu. [18] Huniokoa nikawa salama katika vita vilivyopangwa dhidi yangu, ingawa watu wengi hunipinga. [19] Mungu anayemiliki milele, atawasikia na kuwaadhibu, watu ambao hawabadilishi njia zao, wala hawana hofu ya Mungu. [20] Mwenzangu hushambulia rafiki zake, naye huvunja agano lake. [21] Mazungumzo yake ni laini kama siagi, hata hivyo vita vimo moyoni mwake. Maneno yake ni mororo kuliko mafuta, hata hivyo ni upanga mkali uliofutwa. [22] Mtwike BWANA fadhaa zako, naye atakutegemeza, hatamwacha kamwe mwenye haki wake aanguke. [23] Lakini wewe, Ee Mungu, utawashusha waovu katika shimo la uharibifu. Wenye kiu ya kumwaga damu na wenye hila, hawataishi nusu ya siku zao. Lakini mimi ninakutumaini wewe.