[1] Mwenye Nguvu, Mungu, BWANA, asema na kuiita dunia, tangu mawio ya jua hadi mahali pake liendapo kutua. [2] Kutoka Sayuni, penye uzuri mkamilifu, Mungu anaangaza. [3] Mungu wetu anakuja na hatakaa kimya, moto uteketezao unamtangulia, akiwa amezungukwa na tufani kali. [4] Anaziita mbingu zilizo juu, na nchi, ili aweze kuwahukumu watu wake: [5] “Nikusanyieni watu wangu waliowekwa wakfu, waliofanya agano nami kwa dhabihu.” [6] Nazo mbingu zinatangaza haki yake, kwa maana Mungu mwenyewe ni hakimu. [7] “Sikieni, enyi watu wangu, nami nitasema, ee Israeli, nami nitashuhudia dhidi yenu: Mimi ndimi Mungu, Mungu wenu. [8] Sikukemei kwa sababu ya dhabihu zako, au sadaka zako za kuteketezwa, ambazo daima ziko mbele zangu. [9] Sina haja ya fahali wa banda lako, au mbuzi wa zizi lako. [10] Kwa maana kila mnyama wa msituni ni wangu, na pia makundi ya mifugo juu ya vilima elfu. [11] Ninamjua kila ndege mlimani, nao viumbe wa kondeni ni wangu. [12] Kama ningekuwa na njaa, nisingewaambia ninyi, kwa maana ulimwengu ni wangu, pamoja na vyote vilivyomo ndani yake. [13] Je, mimi hula nyama ya mafahali au kunywa damu ya mbuzi? [14] Toa sadaka za shukrani kwa Mungu, timiza nadhiri zako kwake Yeye Aliye Juu Sana, [15] na uniite siku ya taabu; nami nitakuokoa, nawe utanitukuza.” [16] Lakini kwake mtu mwovu, Mungu asema: “Una haki gani kunena sheria zangu au kuchukua agano langu midomoni mwako? [17] Unachukia mafundisho yangu na kuyatupa maneno yangu nyuma yako. [18] Unapomwona mwizi, unaungana naye, unapiga kura yako pamoja na wazinzi. [19] Unakitumia kinywa chako kwa mabaya na kuuongoza ulimi wako kwa hila. [20] Wanena daima dhidi ya ndugu yako na kumsingizia mwana wa mama yako. [21] Mambo haya unayafanya, nami nimekaa kimya, ukafikiri Mimi nami ni kama wewe. Lakini nitakukemea na kuweka mashtaka mbele yako. [22] “Yatafakarini haya, ninyi mnaomsahau Mungu, ama sivyo nitawararua vipande vipande, wala hapatakuwepo na yeyote wa kuwaokoa: [23] Atoaye dhabihu za shukrani ananiheshimu mimi, naye aiandaa njia yake ili nimwonyeshe wokovu wa Mungu.”