[1] Ee Mungu, unihurumie, kwa kadiri ya upendo wako usiokoma, kwa kadiri ya huruma yako kuu, uyafute makosa yangu. [2] Unioshe na uovu wangu wote na unitakase dhambi yangu. [3] Kwa maana ninajua makosa yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima. [4] Dhidi yako, wewe peke yako, nimetenda dhambi na kufanya yaliyo mabaya machoni pako, ili uthibitike kuwa wa kweli unenapo, na kuwa na haki utoapo hukumu. [5] Hakika mimi nilizaliwa mwenye dhambi, mwenye dhambi tangu nilipotungwa mimba kwa mama yangu. [6] Hakika wewe wapendezwa na kweli itokayo moyoni, ndani sana ya moyo wangu wanifundisha hekima. [7] Nioshe kwa hisopo, nami nitakuwa safi, unisafishe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji. [8] Unipe kusikia furaha na shangwe, mifupa uliyoiponda na ifurahi. [9] Ufiche uso wako usizitazame dhambi zangu, na uufute uovu wangu wote. [10] Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho ya uthabiti ndani yangu. [11] Usinitupe kutoka mbele zako wala kuniondolea Roho wako Mtakatifu. [12] Unirudishie tena furaha ya wokovu wako, unipe roho ya utii, ili initegemeze. [13] Ndipo nitakapowafundisha wakosaji njia zako, na wenye dhambi watakugeukia wewe. [14] Ee Mungu, Mungu uniokoaye, niokoe na hatia ya kumwaga damu, nao ulimi wangu utaimba juu ya haki yako. [15] Ee BWANA, fungua midomo yangu, na kinywa changu kitatangaza sifa zako. [16] Wewe hupendezwi na dhabihu, au ningaliileta, hufurahii sadaka za kuteketezwa. [17] Bali dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika, moyo uliovunjika wenye toba, Ee Mungu, hutaudharau. [18] Kwa wema wa radhi yako uifanye Sayuni istawi, ukazijenge upya kuta za Yerusalemu. [19] Hapo ndipo kutakapokuwa na dhabihu za haki, sadaka nzima za kuteketezwa za kukupendeza sana, pia mafahali watatolewa madhabahuni mwako.