[1] Sikieni haya, enyi mataifa yote, sikilizeni, ninyi wote mkaao dunia hii. [2] Wakubwa kwa wadogo, matajiri na maskini pamoja: [3] Kinywa changu kitasema maneno ya hekima, usemi wa moyo wangu utatoa ufahamu. [4] Nitatega sikio langu nisikilize mithali, nitafafanua kitendawili kwa zeze: [5] Kwa nini niogope siku mbaya zinapokuja, wakati wadanganyifu waovu wanaponizunguka, [6] wale wanaotegemea mali zao na kujivunia utajiri wao mwingi? [7] Hakuna mwanadamu awaye yote awezaye kuukomboa uhai wa mwingine, au kumpa Mungu fidia kwa ajili yake. [8] Fidia ya uhai ni gharama kubwa, hakuna malipo yoyote yanayotosha, [9] ili kwamba aishi milele na asione uharibifu. [10] Wote wanaona kwamba watu wenye hekima hufa; wajinga na wapumbavu vivyo hivyo huangamia na kuwaachia wengine mali zao. [11] Makaburi yao yatabaki kuwa nyumba zao za milele, makao yao vizazi vyote; ingawa walikuwa na mashamba na kuyaita kwa majina yao. [12] Lakini mwanadamu, licha ya utajiri wake, hadumu; anafanana na mnyama aangamiaye. [13] Hii ndiyo hatima ya wale wanaojitumainia wenyewe, pia ya wafuasi wao, waliothibitisha misemo yao. [14] Kama kondoo, wamewekewa kwenda kaburini, nacho kifo kitawala. Wanyofu watawatawala asubuhi, maumbile yao yataozea kaburini, mbali na majumba yao makubwa ya fahari. [15] Lakini Mungu atakomboa uhai wangu na kaburi, hakika atanichukua kwake. [16] Usitishwe mtu anapotajirika, fahari ya nyumba yake inapoongezeka, [17] kwa maana hatachukua chochote atakapokufa, fahari yake haitashuka pamoja naye. [18] Ingawa alipokuwa akiishi alijihesabu kuwa heri, na wanadamu wanakusifu unapofanikiwa, [19] atajiunga na kizazi cha baba zake, ambao hawataona kamwe nuru ya uzima. [20] Mwanadamu mwenye utajiri bila ufahamu ni kama wanyama waangamiao.