[1] BWANA ni mkuu, anayestahili kusifiwa sana, katika mji wa Mungu wetu, mlima wake mtakatifu. [2] Ni mzuri katika kuinuka kwake juu sana, furaha ya dunia yote. Kama vilele vya juu sana vya Safoni ni Mlima Sayuni, mji wa Mfalme Mkuu. [3] Mungu yuko katika ngome zake; amejionyesha mwenyewe kuwa ngome yake. [4] Wakati wafalme walipounganisha nguvu, waliposonga mbele pamoja, [5] walimwona nao wakashangaa, wakakimbia kwa hofu. [6] Kutetemeka kuliwashika huko, maumivu kama ya mwanamke mwenye utungu wa kuzaa. [7] Uliwaangamiza kama meli za Tarshishi zilizovunjwa na upepo wa mashariki. [8] Kama tulivyokuwa tumesikia, ndivyo tulivyoona katika mji wa BWANA Mwenye Nguvu Zote, katika mji wa Mungu wetu: Mungu ataufanya uwe salama milele. [9] Ee Mungu, hekaluni mwako tunatafakari upendo wako usiokoma. [10] Ee Mungu, kama jina lako lilivyo, sifa zako zinafika hadi miisho ya dunia, mkono wako wa kuume umejazwa na haki. [11] Mlima Sayuni unashangilia, vijiji vya Yuda vinafurahi kwa sababu ya hukumu zako. [12] Tembeeni katika Sayuni, uzungukeni mji, hesabuni minara yake; [13] yatafakarini vyema maboma yake, angalieni ngome zake, ili mpate kusimulia habari zake kwa kizazi kijacho. [14] Kwa kuwa huyu Mungu ni Mungu wetu milele na milele; atakuwa kiongozi wetu hata mwisho.