[1] Moyo wangu umesisimuliwa na jambo jema ninapomsimulia mfalme mabeti yangu; ulimi wangu ni kalamu ya mwandishi stadi. [2] Wewe ni bora kuliko watu wengine wote na midomo yako imepakwa neema, kwa kuwa Mungu amekubariki milele. [3] Jifunge upanga wako pajani mwako, ee mwenye nguvu, jivike fahari na utukufu. [4] Katika fahari yako, songa mbele kwa ushindi, kwa ajili ya kweli, unyenyekevu na haki, mkono wako wa kuume na uonyeshe matendo ya kutisha. [5] Mishale yako mikali na ichome mioyo ya adui za mfalme, mataifa na yaanguke chini ya nyayo zako. [6] Ee Mungu, kiti chako cha enzi kitadumu milele na milele, fimbo ya utawala wa haki itakuwa fimbo ya utawala wa ufalme wako. [7] Unaipenda haki na kuchukia uovu; kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekuweka juu ya wenzako, kwa kukupaka mafuta ya furaha. [8] Mavazi yako yote yana harufu nzuri ya manemane, udi na mdalasini; kutoka kwenye majumba ya kifalme yaliyopambwa kwa pembe za ndovu, sauti za vinanda vya nyuzi zinakufanya ufurahi. [9] Binti za wafalme ni miongoni mwa wanawake wako waheshimiwa; kuume kwako yupo bibi arusi malkia aliyevaa dhahabu ya Ofiri. [10] Sikiliza, ewe binti, fikiri na utege sikio: Sahau watu wako na nyumba ya baba yako. [11] Mfalme ameshangazwa na uzuri wako; mheshimu, kwa kuwa yeye ni bwana wako. [12] Binti wa Tiro atakuletea zawadi, watu wenye utajiri watatafuta upendeleo wako. [13] Utukufu wote una binti mfalme katika chumba chake; vazi lake limefumwa kwa nyuzi za dhahabu. [14] Anaongozwa kwa mfalme, akiwa amevalia mavazi yaliyotariziwa, mabikira wenzake wanamfuata na wanaletwa kwako. [15] Wanaingizwa ndani kwa shangwe na furaha, na kuingia katika jumba la mfalme. [16] Wana wenu watachukua nafasi za baba zenu, mtawafanya wakuu katika nchi yote. [17] Nitadumisha kumbukumbu lako katika vizazi vyote, kwa hiyo mataifa watakusifu milele na milele.