[1] Ee Mungu, tumesikia kwa masikio yetu, baba zetu wametueleza yale uliyotenda katika siku zao, siku za kale. [2] Kwa mkono wako uliwafukuza mataifa na ukawapanda baba zetu, uliangamiza mataifa na kuwastawisha baba zetu. [3] Sio kwa upanga wao waliipata nchi, wala si mkono wao uliwapatia ushindi; ilikuwa ni kitanga cha mkono wako wa kuume, na nuru ya uso wako, kwa kuwa uliwapenda. [4] Wewe ni mfalme wangu na Mungu wangu, unayeamuru ushindi kwa Yakobo. [5] Kwa uwezo wako tunawasukuma nyuma watesi wetu; kwa jina lako tunawakanyaga adui zetu. [6] Siutumaini upinde wangu, upanga wangu hauniletei ushindi; [7] bali wewe unatupa ushindi juu ya adui zetu, unawaaibisha watesi wetu. [8] Katika Mungu wetu tunajivuna mchana kutwa, nasi tutalisifu jina lako milele. [9] Lakini sasa umetukataa na kutudhili, wala huendi tena na jeshi letu. [10] Umetufanya turudi nyuma mbele ya adui, nao watesi wetu wametuteka nyara. [11] Umetuacha tutafunwe kama kondoo na umetutawanya katika mataifa. [12] Umewauza watu wako kwa fedha kidogo, wala hukupata faida yoyote kwa mauzo yao. [13] Umetufanya lawama kwa jirani zetu, dharau na dhihaka kwa wale wanaotuzunguka. [14] Umetufanya kuwa mithali miongoni mwa mataifa, mataifa hutikisa vichwa vyao. [15] Fedheha yangu iko mbele yangu mchana kutwa, na uso wangu umejaa aibu tele, [16] kwa ajili ya dhihaka ya wale wanaonilaumu na kunitukana, kwa sababu ya adui, ambaye anatamani kulipiza kisasi. [17] Hayo yote yametutokea, ingawa tulikuwa hatujakusahau wala hatujaenda kinyume na agano lako. [18] Mioyo yetu ilikuwa haijarudi nyuma; nyayo zetu zilikuwa hazijaiacha njia yako. [19] Lakini ulituponda na kutufanya makao ya mbweha, na ukatufunika kwa giza nene. [20] Kama tungalikuwa tumelisahau jina la Mungu wetu au kunyooshea mikono yetu kwa mungu mgeni, [21] je, Mungu hangaligundua hili, kwa kuwa anazijua siri za moyo? [22] Hata hivyo kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa; tumehesabiwa kama kondoo wa kuchinjwa. [23] Amka, Ee BWANA! Kwa nini unalala? Zinduka! Usitukatae milele. [24] Kwa nini unauficha uso wako na kusahau taabu na mateso yetu? [25] Tumeshushwa hadi mavumbini, miili yetu imegandamana na ardhi. [26] Inuka na utusaidie, utukomboe kwa sababu ya upendo wako usio na mwisho.