Zaburi 37:1-40 ONEN
[1] Usisumbuke kwa ajili ya watendao maovu, wala usiwaonee wivu watendao mabaya, [2] kwa maana kama majani watanyauka mara, kama mimea ya kijani watakufa mara. [3] Mtumaini BWANA na utende yaliyo mema; Kaa katika nchi ukafurahie malisho salama. [4] Jifurahishe katika BWANA naye atakupa haja za moyo wako. [5] Mkabidhi BWANA njia yako, mtumaini yeye, naye atatenda hili: [6] Yeye atafanya haki yako ingʼae kama mapambazuko, na hukumu ya shauri lako kama jua la adhuhuri. [7] Tulia mbele za BWANA na umngojee kwa uvumilivu; usisumbuke watu wanapofanikiwa katika njia zao, wanapotekeleza mipango yao miovu. [8] Epuka hasira na uache ghadhabu, usihangaike: itakuongoza tu kutenda uovu. [9] Kwa maana waovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini BWANA watairithi nchi. [10] Bado kitambo kidogo, nao waovu hawataonekana, ingawa utawatafuta, hawataonekana. [11] Bali wanyenyekevu watairithi nchi na wafurahie amani tele. [12] Waovu hula njama dhidi ya wenye haki na kuwasagia meno, [13] bali Bwana huwacheka waovu, kwa sababu anajua siku yao inakuja. [14] Waovu huchomoa upanga na kupinda upinde, ili wawaangushe maskini na wahitaji, kuwachinja wale ambao njia zao ni nyofu. [15] Lakini panga zao zitachoma mioyo yao wenyewe, na pinde zao zitavunjwa. [16] Bora kidogo walicho nacho wenye haki kuliko wingi wa mali wa waovu wengi; [17] kwa maana nguvu za waovu zitavunjwa, lakini BWANA humtegemeza mwenye haki. [18] BWANA anazifahamu siku za wanyofu, na urithi wao utadumu milele. [19] Siku za maafa hawatanyauka, siku za njaa watafurahia wingi wa vitu. [20] Lakini waovu wataangamia: Adui za BWANA watakuwa kama uzuri wa mashamba, watatoweka, watatoweka kama moshi. [21] Waovu hukopa na hawalipi, bali wenye haki hutoa kwa ukarimu. [22] Wale wanaobarikiwa na BWANA watairithi nchi, bali wale anaowalaani watakatiliwa mbali. [23] Kama BWANA akipendezwa na njia ya mtu, yeye huimarisha hatua zake, [24] ajapojikwaa, hataanguka, kwa maana BWANA humtegemeza kwa mkono wake. [25] Nilikuwa kijana na sasa ni mzee, lakini sijaona kamwe wenye haki wameachwa au watoto wao wakiombaomba chakula. [26] Wakati wote ni wakarimu na hukopesha bila masharti. Watoto wao watabarikiwa. [27] Acha ubaya na utende wema, nawe utaishi katika nchi milele. [28] Kwa kuwa BWANA huwapenda wenye haki naye hatawaacha waaminifu wake. Watalindwa milele, lakini uzao wa waovu utakatiliwa mbali. [29] Wenye haki watairithi nchi, na kuishi humo milele. [30] Kinywa cha mwenye haki hutamka hekima, nao ulimi wake huzungumza lililo haki. [31] Sheria ya Mungu wake imo moyoni mwake; nyayo zake hazitelezi. [32] Watu waovu huvizia wenye haki, wakitafuta kuwaua; [33] lakini BWANA hatawaacha mikononi mwao wala hatawaacha wahukumiwe kuwa wakosa wanaposhtakiwa. [34] Mngojee BWANA, na uishike njia yake. Naye atakutukuza uirithi nchi, waovu watakapokatiliwa mbali, utaliona hilo. [35] Nimemwona mtu mwovu na mkatili akistawi kama mwerezi wa Lebanoni, [36] lakini alitoweka mara na hakuonekana, ingawa nilimtafuta, hakupatikana. [37] Watafakari watu wasio na hatia, wachunguze watu wakamilifu, kuna mafanikio kwa mtu apendaye amani. [38] Lakini watenda dhambi wote wataangamizwa, mafanikio yao yatakatiliwa mbali. [39] Wokovu wa wenye haki hutoka kwa BWANA, yeye ni ngome yao wakati wa shida. [40] BWANA huwasaidia na kuwaokoa, huwaokoa kutoka kwa waovu na kuwahifadhi, kwa maana wanamkimbilia.
