Zaburi 36:1-12 ONEN

[1] Kuna neno moyoni mwangu kuhusu hali ya dhambi ya mwovu. Hakuna hofu ya Mungu mbele ya macho yake. [2] Kwa kuwa machoni pake mwenyewe hujisifu mno hata hawezi kugundua au kuichukia dhambi yake. [3] Maneno ya kinywa chake ni maovu na ya udanganyifu, ameacha kuwa mwenye hekima na kutenda mema. [4] Hata kitandani mwake hupanga hila mbaya, hujitia katika njia ya dhambi na hakatai lililo baya. [5] Upendo wako, Ee BWANA, unafika hadi mbinguni, uaminifu wako hadi kwenye anga. [6] Haki yako ni kama milima mikubwa, hukumu zako ni kama kilindi kikuu. Ee BWANA, wewe huwahifadhi mwanadamu na mnyama. [7] Upendo wako usiokoma ni wa thamani mno! Watu wakuu na wadogo hujificha uvulini wa mbawa zako. [8] Wanajifurahisha katika wingi nyumbani mwako, nawe utawanywesha katika mto wa furaha zako. [9] Kuwa pamoja nawe ni kijito cha uzima, katika nuru yako twaona nuru. [10] Dumisha upendo wako kwa wale wanaokujua wewe, haki yako kwa wale walio wanyofu wa moyo. [11] Mguu wa mwenye kiburi usije dhidi yangu, wala mkono wa mwovu usinifukuze. [12] Angalia jinsi watenda mabaya walivyoanguka: wametupwa chini, hawawezi kuinuka!

About this translation

Life Bible app icon
Get the Life Bible app Read offline, sync highlights and notes, and study with your library on any device.