[1] Ee BWANA, usinikemee katika hasira yako, wala kuniadhibu katika ghadhabu yako. [2] Kwa kuwa mishale yako imenichoma, na mkono wako umenishukia. [3] Hakuna afya mwilini mwangu kwa sababu ya ghadhabu yako, mifupa yangu haina uzima kwa sababu ya dhambi zangu. [4] Maovu yangu yamenifunika kama mzigo usiochukulika. [5] Majeraha yangu yameoza na yananuka, kwa sababu ya upumbavu wa dhambi zangu. [6] Nimeinamishwa chini na kushushwa sana, mchana kutwa nazunguka nikiomboleza. [7] Viuno vyangu vimejaa maumivu yaunguzayo, hakuna afya mwilini mwangu. [8] Nimedhoofika na kupondwa kabisa, nasononeka kwa maumivu makuu ya moyoni. [9] Ee BWANA, yote ninayoyaonea shauku yako wazi mbele zako, kutamani kwangu sana hakufichiki mbele zako. [10] Moyo wangu unapigapiga, nguvu zangu zimeniishia; hata macho yangu yametiwa giza. [11] Rafiki na wenzangu wananikwepa kwa sababu ya majeraha yangu; majirani zangu wanakaa mbali nami. [12] Wale wanaotafuta uhai wangu wanatega mitego yao, wale ambao wangetaka kunidhuru huongea juu ya maangamizi yangu; hufanya shauri la hila mchana kutwa. [13] Mimi ni kama mtu kiziwi, asiyeweza kusikia, ni kama bubu, asiyeweza kufungua kinywa chake, [14] nimekuwa kama mtu asiyesikia, ambaye kinywa chake hakiwezi kutoa jibu. [15] Ee BWANA, ninakungojea wewe, Ee Bwana Mungu wangu, utajibu. [16] Kwa kuwa nilisema, “Usiwaache wafurahie, wala wasijitukuze juu yangu mguu wangu unapoteleza.” [17] Kwa maana ninakaribia kuanguka, na maumivu yangu yananiandama siku zote. [18] Naungama uovu wangu, ninataabishwa na dhambi yangu. [19] Wengi ni wale ambao ni adui zangu hodari, wale wanaonichukia bila sababu ni wengi. [20] Wanaolipa maovu kwa wema wangu hunisingizia ninapofuata lililo jema. [21] Ee BWANA, usiniache, usiwe mbali nami, Ee Mungu wangu. [22] Ee Bwana Mwokozi wangu, uje upesi kunisaidia.