Zaburi 35:1-28 ONEN
[1] Ee BWANA, pingana na wale wanaopingana nami, upigane na hao wanaopigana nami. [2] Chukua ngao na kigao. Inuka unisaidie. [3] Inua mkuki wako na fumo lako dhidi ya hao wanaonifuatia. Iambie nafsi yangu, “Mimi ni wokovu wako.” [4] Wafedheheshwe na waaibishwe wale wanaotafuta uhai wangu. Wanaofanya shauri kuniangamiza warudishwe nyuma kwa hofu. [5] Wawe kama makapi yapeperushwayo na upepo, malaika wa BWANA akiwafukuza. [6] Njia yao na iwe giza na ya utelezi, malaika wa BWANA akiwafuatilia. [7] Kwa vile walinifichia wavu wao bila sababu, na bila sababu wamenichimbia shimo, [8] maafa na yawapate ghafula: wavu walionifichia na uwatege wenyewe, na waanguke katika shimo hilo, kwa maangamizo yao. [9] Ndipo nafsi yangu itashangilia katika BWANA na kuufurahia wokovu wake. [10] Nitapaza sauti yangu nikisema, “Ni nani aliye kama wewe, Ee BWANA? Wewe huwaokoa maskini kutokana na wale walio na nguvu kuliko wao, maskini na mhitaji kutokana na wanaowanyangʼanya!” [11] Mashahidi wakatili wanainuka, wananiuliza mambo nisiyoyajua. [12] Wananilipa baya kwa jema na kuiacha nafsi yangu ukiwa. [13] Lakini walipokuwa wagonjwa, nilivaa nguo ya gunia na nikajinyenyekesha kwa kufunga. Maombi yangu yaliponirudia bila kujibiwa, [14] niliendelea kuomboleza kama vile wao ni rafiki au ndugu. Niliinamisha kichwa chini kwa huzuni kama ninayemwombolezea mama yangu. [15] Lakini nilipojikwaa, walikusanyika kwa shangwe; washambuliaji walijikusanya dhidi yangu bila mimi kujua. Walinisingizia pasipo kukoma. [16] Kama watu wasiomcha Mungu, wamenidhihaki, wamenisagia meno. [17] Ee BWANA, utatazama mpaka lini? Niokoe maisha yangu na maangamizi yao, uhai wangu wa thamani kutokana na simba hawa. [18] Nami nitakushukuru mbele ya kusanyiko kubwa, nitakusifu katikati ya watu wengi. [19] Usiwaache wale wanaonisimanga, wale ambao ni adui zangu bila sababu; usiwaache wale ambao ni adui zangu bila sababu wakonyeze jicho kwa hila. [20] Hawazungumzi kwa amani, bali wanatunga mashtaka ya uongo dhidi ya wale wanaoishi kwa utulivu katika nchi. [21] Hunifumbulia vinywa vyao wakisema, “Aha! Aha! Kwa macho yetu wenyewe tumeliona.” [22] Ee BWANA, umeona hili, usiwe kimya. Usiwe mbali nami, Ee BWANA. [23] Amka, inuka unitetee! Unipiganie Mungu wangu na Bwana wangu. [24] Nihukumu kwa haki yako, Ee BWANA Mungu wangu, sawasawa na haki yako; usiwaache wakusimange. [25] Usiwaache wafikiri, “Aha, hili ndilo tulilotaka!” Au waseme, “Tumemmeza.” [26] Wote wanaofurahia dhiki yangu waaibishwe na wachanganyikiwe; hao wanaojiinua dhidi yangu wavikwe aibu na dharau. [27] Wale wanaofurahia hukumu yangu ya haki wapige kelele za shangwe na furaha; hebu waseme siku zote, “BWANA atukuzwe, ambaye amefurahia mafanikio ya mtumishi wake.” [28] Ulimi wangu utanena haki yako na sifa zako mchana kutwa.
