[1] Nitamtukuza BWANA nyakati zote, sifa zake zitakuwa midomoni mwangu siku zote. [2] Nafsi yangu itajisifu katika BWANA, walioonewa watasikia na wafurahi. [3] Mtukuzeni BWANA pamoja nami, naam, na tulitukuze jina lake pamoja. [4] Nilimtafuta BWANA naye akanijibu, akaniokoa kwenye hofu zangu zote. [5] Wale wamtazamao hutiwa nuru, nyuso zao hazifunikwi na aibu kamwe. [6] Maskini huyu alimwita BWANA, naye akamsikia, akamwokoa katika taabu zake zote. [7] Malaika wa BWANA hufanya kituo akiwazunguka wale wamchao, naye huwaokoa. [8] Onjeni mwone kwamba BWANA ni mwema, heri mtu yule anayemkimbilia. [9] Mcheni BWANA enyi watakatifu wake, kwa maana wale wamchao hawapungukiwi na chochote. [10] Wana simba wenye nguvu hutindikiwa na kuona njaa, bali wale wamtafutao BWANA hawatakosa kitu chochote kilicho chema. [11] Njooni, watoto wangu, mnisikilize, nitawafundisha kumcha BWANA. [12] Yeyote kati yenu anayependa uzima na kutamani kuziona siku nyingi njema, [13] basi auzuie ulimi wake na mabaya, na midomo yake kutokana na kusema uongo. [14] Aache uovu, atende mema, aitafute amani na kuifuatilia. [15] Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake yako makini kusikiliza kilio chao. [16] Uso wa BWANA uko kinyume na watendao maovu, ili kufuta kumbukumbu lao duniani. [17] Wenye haki hulia, naye BWANA huwasikia, huwaokoa katika taabu zao zote. [18] BWANA yu karibu na waliovunjika moyo, na huwaokoa waliopondeka roho. [19] Mwenye haki ana mateso mengi, lakini BWANA humwokoa nayo yote, [20] huhifadhi mifupa yake yote, hata mmoja hautavunjika. [21] Ubaya utamuua mtu mwovu, nao adui za mwenye haki watahukumiwa. [22] BWANA huwakomboa watumishi wake, yeyote anayemkimbilia yeye hatahukumiwa kamwe.