[1] Mwimbieni BWANA kwa furaha, enyi wenye haki; kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo. [2] Msifuni BWANA kwa kinubi, mwimbieni sifa kwa zeze la nyuzi kumi. [3] Mwimbieni wimbo mpya; pigeni kwa ustadi, na mpaze sauti za shangwe. [4] Maana neno la BWANA ni haki na kweli, ni mwaminifu kwa yote atendayo. [5] BWANA hupenda uadilifu na haki; dunia imejaa upendo wake usiokoma. [6] Kwa neno la BWANA mbingu ziliumbwa, jeshi lao la angani kwa pumzi ya kinywa chake. [7] Ameyakusanya maji ya bahari kama kwenye chungu; vilindi vya bahari ameviweka katika ghala. [8] Dunia yote na imwogope BWANA, watu wote wa dunia wamche. [9] Kwa maana Mungu alisema, na ikawa, aliamuru na ikasimama imara. [10] BWANA huzuia mipango ya mataifa, hupinga makusudi ya mataifa. [11] Lakini mipango ya BWANA inasimama imara milele, makusudi ya moyo wake kwa vizazi vyote. [12] Heri taifa ambalo BWANA ni Mungu wao, watu ambao aliwachagua kuwa urithi wake. [13] Kutoka mbinguni BWANA hutazama chini na kuwaona wanadamu wote; [14] kutoka maskani mwake huwaangalia wote wakaao duniani: [15] yeye ambaye huumba mioyo yao wote, ambaye huangalia kila kitu wanachokitenda. [16] Hakuna mfalme aokokaye kwa ukubwa wa jeshi lake; hakuna shujaa aokokaye kwa wingi wa nguvu zake. [17] Farasi ni tumaini la bure kwa wokovu, licha ya nguvu zake nyingi, hawezi kuokoa. [18] Lakini macho ya BWANA yako kwa wale wamchao, kwa wale tumaini lao liko katika upendo wake usio na kikomo, [19] ili awaokoe na mauti, na kuwahifadhi wakati wa njaa. [20] Sisi tunamngojea BWANA kwa matumaini, yeye ni msaada wetu na ngao yetu. [21] Mioyo yetu humshangilia, kwa maana tunalitumainia jina lake takatifu. [22] Upendo wako usio na mwisho ukae juu yetu, Ee BWANA, tunapoliweka tumaini letu kwako.