[1] Heri mtu yule ambaye amesamehewa makosa yake, ambaye dhambi zake zimefunikwa. [2] Heri mtu yule ambaye BWANA hamhesabii dhambi, na ambaye rohoni mwake hamna udanganyifu. [3] Niliponyamaza, mifupa yangu ilichakaa kwa kulia kwa maumivu makali mchana kutwa. [4] Usiku na mchana mkono wako ulinilemea, nguvu zangu zilinyonywa kama vile katika joto la kiangazi. [5] Kisha nilikujulisha dhambi yangu wala sikuficha uovu wangu. Nilisema, “Nitaungama makosa yangu kwa BWANA.” Ndipo uliponisamehe hatia ya dhambi yangu. [6] Kwa hiyo kila mtu mcha Mungu akuombe wakati unapopatikana, hakika maji makuu yatakapofurika hayatamfikia yeye. [7] Wewe ndiwe mahali pangu pa kujificha, utaniepusha na taabu na kunizunguka kwa nyimbo za wokovu. [8] Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri na kukuangalia. [9] Usiwe kama farasi au nyumbu wasio na akili, ambao ni lazima waongozwe kwa lijamu na hatamu la sivyo hawatakukaribia. [10] Mtu mwovu ana taabu nyingi, bali upendo usio na kikomo wa BWANA unamzunguka mtu anayemtumaini. [11] Shangilieni katika BWANA na mfurahi, enyi wenye haki! Imbeni, nyote mlio wanyofu wa moyo!