Zaburi 31:1-24 ONEN
[1] Ee BWANA, nimekukimbilia wewe, usiache nikaaibika kamwe, kwa haki yako uniokoe. [2] Nitegee sikio lako, uje uniokoe haraka; uwe kwangu mwamba wa kimbilio, ngome imara ya kuniokoa. [3] Kwa kuwa wewe ni mwamba wangu na ngome yangu, uniongoze na kunilinda kwa ajili ya jina lako. [4] Uniepushe na mtego niliotegewa, maana wewe ndiwe kimbilio langu. [5] Ninaikabidhi roho yangu mikononi mwako, unikomboe Ee BWANA, uliye Mungu wa kweli. [6] Ninawachukia wale wanaongʼangʼania sanamu batili; mimi ninamtumaini BWANA. [7] Nitafurahia na kushangilia upendo wako, kwa kuwa uliona mateso yangu na ulijua maumivu ya nafsi yangu. [8] Hukunikabidhi kwa adui yangu bali umeiweka miguu yangu mahali penye nafasi. [9] Ee BWANA unihurumie, kwa kuwa niko kwenye shida; macho yangu yanafifia kwa huzuni, nafsi yangu na mwili wangu kwa sikitiko. [10] Maisha yangu yamedhoofika kwa majonzi, naam, miaka yangu kwa kulia kwa maumivu makali; nguvu zangu zinaisha kwa ajili ya mateso, na mifupa yangu inachakaa. [11] Kwa sababu ya adui zangu wote, nimedharauliwa kabisa na jirani zangu, hata kwa rafiki zangu nimekuwa tisho, wale wanionao barabarani hunikimbia. [12] Nimesahaulika miongoni mwao kama mtu aliyekufa, nimekuwa kama chombo cha mfinyanzi kilichovunjika. [13] Kwa maana nimesikia maneno niliyosingiziwa na wengi; vitisho viko pande zote; kwa kuwa wamefanya mashauri dhidi yangu, na kula njama kuniua. [14] Lakini mimi ninakutumaini wewe peke yako, Ee BWANA; nimesema, “Wewe ndiwe Mungu wangu.” [15] Siku za maisha yangu ziko mikononi mwako, uniokoe mikononi mwa adui zangu na wale wanifuatiao. [16] Mwangazie mtumishi wako uso wako, uniokoe kwa ajili ya upendo wako usiokoma. [17] Usiniache niaibike, Ee BWANA, kwa maana nimekulilia wewe, bali waovu waaibishwe na kunyamazishwa Kuzimu. [18] Midomo yao isemayo uongo na inyamazishwe, kwa maana kwa kiburi na dharau wao husema kwa majivuno dhidi ya wenye haki. [19] Tazama jinsi ulivyo mkuu wema wako, uliowawekea akiba wakuchao, ambao huwapa wale wakukimbiliao machoni pa watu. [20] Unawahifadhi katika uvuli wa uwepo wako kutokana na hila za wanadamu; katika makao yako huwaweka salama kutokana na ndimi za mashtaka. [21] Atukuzwe BWANA, kwa kuwa amenionyesha upendo wake wa ajabu nilipokuwa katika mji uliozingirwa. [22] Katika hofu yangu nilisema, “Nimekatiliwa mbali na macho yako!” Hata hivyo ulisikia kilio changu ukanihurumia nilipokuita unisaidie. [23] Mpendeni BWANA ninyi watakatifu wake wote! BWANA huwahifadhi waaminifu, lakini wenye kiburi huwalipiza kikamilifu. [24] Kuweni hodari na mjipe moyo, ninyi nyote mnaomtumaini BWANA.
