[1] Mpeni BWANA, enyi mashujaa, mpeni BWANA utukufu na nguvu. [2] Mpeni BWANA utukufu unaostahili jina lake; mwabuduni BWANA katika uzuri wa utakatifu wake. [3] Sauti ya BWANA iko juu ya maji; Mungu wa utukufu hupiga radi, BWANA hupiga radi juu ya maji makuu. [4] Sauti ya BWANA ina nguvu; sauti ya BWANA ni tukufu. [5] Sauti ya BWANA huvunja mierezi; BWANA huvunja vipande vipande mierezi ya Lebanoni. [6] Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama, Sirioni urukaruke kama mwana nyati. [7] Sauti ya BWANA hupiga kwa miali ya umeme wa radi. [8] Sauti ya BWANA hutikisa jangwa; BWANA hutikisa Jangwa la Kadeshi. [9] Sauti ya BWANA huzalisha ayala, na huuacha msitu wazi. Hekaluni mwake wote wasema, “Utukufu!” [10] BWANA huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika; BWANA ametawazwa kuwa Mfalme milele. [11] BWANA huwapa watu wake nguvu; BWANA huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.