[1] Ninakuita wewe, Ee BWANA, Mwamba wangu; usiwe kwangu kama kiziwi. Kwa sababu ukinyamaza nitafanana na walioshuka shimoni. [2] Sikia kilio changu unihurumie ninapokuita kwa ajili ya msaada, niinuapo mikono yangu kuelekea Patakatifu pa Patakatifu pako. [3] Usiniburute pamoja na waovu, pamoja na hao watendao mabaya, ambao huzungumza na jirani zao maneno mazuri, lakini mioyoni mwao wameficha chuki. [4] Walipe sawasawa na matendo yao, sawasawa na matendo yao maovu; walipe sawasawa na kazi za mikono yao, uwalipe wanavyostahili. [5] Kwa kuwa hawaheshimu kazi za BWANA, na yale ambayo mikono yake imetenda, atawabomoa na kamwe hatawajenga tena. [6] BWANA asifiwe, kwa maana amesikia kilio changu nikimwomba anihurumie. [7] BWANA ni nguvu zangu na ngao yangu, moyo wangu umemtumaini yeye, nami nimesaidiwa. Moyo wangu unarukaruka kwa furaha nami nitamshukuru kwa wimbo. [8] BWANA ni nguvu ya watu wake, ngome ya wokovu kwa mpakwa mafuta wake. [9] Waokoe watu wako na uubariki urithi wako; uwe mchungaji wao na uwabebe milele.