[1] BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani? BWANA ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani? [2] Waovu watakaposogea dhidi yangu ili wanile nyama yangu, adui zangu na watesi wangu watakaponishambulia, watajikwaa na kuanguka. [3] Hata jeshi linizunguke pande zote, moyo wangu hautaogopa; hata vita vitokee dhidi yangu, hata hapo nitakuwa na ujasiri. [4] Jambo moja ninamwomba BWANA, hili ndilo ninalolitafuta: niweze kukaa nyumbani mwa BWANA siku zote za maisha yangu, niutazame uzuri wa BWANA na kumtafuta hekaluni mwake. [5] Kwa kuwa siku ya shida, atanihifadhi salama katika maskani yake, atanificha uvulini mwa hema yake na kuniweka juu kwenye mwamba. [6] Kisha kichwa changu kitainuliwa juu ya adui zangu wanaonizunguka. Katika maskani yake nitatoa dhabihu kwa kelele za shangwe; nitamwimbia BWANA na kumsifu. [7] Isikie sauti yangu nikuitapo, Ee BWANA, unihurumie na unijibu. [8] Moyo wangu unasema kuhusu wewe, “Utafute uso wake!” Uso wako, BWANA “Nitautafuta.” [9] Usinifiche uso wako, usimkatae mtumishi wako kwa hasira; wewe umekuwa msaada wangu. Usinikatae wala usiniache, Ee Mungu Mwokozi wangu. [10] Hata kama baba yangu na mama wakiniacha, BWANA atanipokea. [11] Nifundishe njia yako, Ee BWANA, niongoze katika njia iliyonyooka kwa sababu ya watesi wangu. [12] Usiniachilie kwa nia za adui zangu, kwa maana mashahidi wa uongo wameinuka dhidi yangu, wakipumua ujeuri. [13] Nami bado nina tumaini hili: nitauona wema wa BWANA katika nchi ya walio hai. [14] Mngojee BWANA, uwe hodari na mwenye moyo mkuu, nawe, umngojee BWANA.