[1] Ee BWANA, nithibitishe katika haki, maana nimeishi maisha yasiyo na lawama; nimemtumainia BWANA bila kusitasita. [2] Ee BWANA, unijaribu, unipime, uuchunguze moyo wangu na mawazo yangu; [3] kwa maana upendo wako uko mbele yangu daima, nami natembea siku zote katika kweli yako. [4] Siketi pamoja na watu wadanganyifu, wala siandamani na wanafiki, [5] ninachukia kusanyiko la watenda mabaya na ninakataa kuketi pamoja na waovu. [6] Ninanawa mikono yangu kwa kuwa sina hatia, naikaribia madhabahu yako, Ee BWANA, [7] nikitangaza sifa yako kwa sauti kubwa, huku nikisimulia matendo yako ya ajabu. [8] Ee BWANA, naipenda nyumba yako mahali unakoishi, mahali ambapo utukufu wako hukaa. [9] Usiiondoe nafsi yangu pamoja na watenda dhambi, wala uhai wangu pamoja na wamwagao damu, [10] ambao mikononi mwao kuna mipango miovu, ambao mikono yao ya kuume imejaa rushwa. [11] Bali mimi ninaishi maisha yasiyo na lawama; nikomboe na unihurumie. [12] Miguu yangu imesimama katika uwanja tambarare; katika kusanyiko kuu nitamsifu BWANA.