[1] Kwako wewe, Ee BWANA, nainua nafsi yangu, [2] ni wewe ninayekutumainia, Ee Mungu wangu. Usiniache niaibike, wala usiache adui zangu wakanishinda. [3] Kamwe hakuna hata mmoja anayekutegemea atakayeaibishwa, bali wataaibishwa wafanyao hila bila sababu. [4] Nionyeshe njia zako, Ee BWANA, nifundishe mapito yako, [5] niongoze katika kweli yako na kunifundisha, kwa maana wewe ni Mungu Mwokozi wangu, nalo tumaini langu liko kwako wakati wote. [6] Kumbuka, Ee BWANA, rehema zako kuu na upendo, kwa maana zimekuwepo tangu zamani. [7] Usizikumbuke dhambi za ujana wangu wala njia zangu za uasi, sawasawa na upendo wako unikumbuke, kwa maana wewe ni mwema, Ee BWANA. [8] BWANA ni mwema na mwenye adili, kwa hiyo huwafundisha wenye dhambi njia zake. [9] Huwaongoza wanyenyekevu katika haki, naye huwafundisha njia yake. [10] Njia zote za BWANA ni za upendo na uaminifu kwa wale wanaoshika shuhuda za agano lake. [11] Ee BWANA, kwa ajili ya jina lako, unisamehe uovu wangu, ijapokuwa ni mwingi. [12] Ni nani basi, mtu yule anayemcha BWANA? Atamfundisha katika njia atakayoichagua kwa ajili yake. [13] Mtu huyo atafanikiwa maishani mwake, nao wazao wake watairithi nchi. [14] Siri ya BWANA iko kwa wale wamchao, yeye huwajulisha agano lake. [15] Macho yangu humwelekea BWANA daima, kwa kuwa yeye peke yake ndiye ataitoa miguu yangu kutoka mtego. [16] Nigeukie na unihurumie, kwa maana mimi ni mpweke na mwenye kuteseka. [17] Shida za moyo wangu zimeongezeka, niokoe katika dhiki yangu. [18] Uangalie mateso na shida zangu na uniondolee dhambi zangu zote. [19] Tazama adui zangu walivyo wengi, pia uone jinsi wanavyonichukia vikali! [20] Uyalinde maisha yangu na uniokoe, usiniache niaibike, kwa maana nimekukimbilia wewe. [21] Uadilifu na uaminifu vinilinde, kwa sababu tumaini langu ni kwako. [22] Ee Mungu, wakomboe Israeli, katika shida zao zote!