[1] Dunia ni mali ya BWANA, na vyote vilivyomo ndani yake, ulimwengu, na wote waishio ndani yake, [2] maana aliiwekea misingi yake baharini na kuifanya imara juu ya maji. [3] Nani awezaye kuupanda mlima wa BWANA? Ni nani awezaye kusimama patakatifu pake? [4] Ni yule mwenye mikono safi na moyo mweupe, yule ambaye hakuinulia sanamu nafsi yake au kuapa kwa kitu cha uongo. [5] Huyo atapokea baraka kutoka kwa BWANA, na hukumu ya haki kutoka kwa Mungu Mwokozi wake. [6] Hiki ndicho kizazi cha wale wamtafutao, wale wautafutao uso wako, Ee Mungu wa Yakobo. [7] Inueni vichwa vyenu, enyi malango, inukeni enyi milango ya kale, ili mfalme wa utukufu apate kuingia. [8] Ni nani huyu Mfalme wa utukufu? Ni BWANA aliye na nguvu na uweza, ni BWANA aliye hodari katika vita. [9] Inueni vichwa vyenu, enyi malango, viinueni juu enyi milango ya kale, ili Mfalme wa utukufu apate kuingia. [10] Ni nani yeye, huyu Mfalme wa utukufu? Ni BWANA Mwenye Nguvu Zote; yeye ndiye Mfalme wa utukufu.