[1] Ee BWANA, mfalme huzifurahia nguvu zako. Tazama jinsi ilivyo kuu furaha yake kwa ushindi unaompa! [2] Umempa haja ya moyo wake na hukumzuilia maombi ya midomo yake. [3] Ulimkaribisha kwa baraka tele na kumvika taji ya dhahabu safi kichwani pake. [4] Alikuomba maisha, nawe ukampa, wingi wa siku milele na milele. [5] Kutokana na ushindi uliompa, utukufu wake ni mkubwa, umeweka juu yake fahari na utukufu. [6] Hakika umempa baraka za milele, umemfanya awe na furaha kwa shangwe ya uwepo wako. [7] Kwa kuwa mfalme anamtumaini BWANA; kwa upendo usiokoma wa Aliye Juu Sana hatatikiswa. [8] Mkono wako utawashika adui zako wote, mkono wako wa kuume utawakamata adui zako. [9] Wakati utakapojitokeza utawafanya kama tanuru ya moto. Katika ghadhabu yake BWANA atawameza, moto wake utawateketeza. [10] Utawaangamiza wazao wao kutoka duniani, uzao wao kutoka wanadamu. [11] Ingawa watapanga mabaya dhidi yako na kutunga hila, hawawezi kufanikiwa, [12] kwa kuwa utawafanya wakimbie utakapowalenga usoni pao kwa mshale kutoka kwenye upinde wako. [13] Ee BWANA, utukuzwe katika nguvu zako, tutaimba na kusifu nguvu zako.