Zaburi 22:1-31 ONEN
[1] Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Kwa nini uko mbali hivyo kuniokoa? Mbali hivyo na maneno ya kuugua kwangu? [2] Ee Mungu wangu, ninalia mchana, lakini hunijibu, hata usiku, sinyamazi. [3] Hata hivyo umesimikwa katika kiti cha enzi kama Uliye Mtakatifu; wewe ni sifa ya Israeli. [4] Kwako wewe baba zetu waliweka tumaini lao, walikutumaini nawe ukawaokoa. [5] Walikulilia wewe na ukawaokoa, walikutegemea wewe nao hawakuaibika. [6] Mimi ni mnyoo wala si mwanadamu, wanaume wamenibeza, na watu wamenidharau. [7] Wote wanionao hunidhihaki, hunivurumishia matusi, wakitikisa vichwa vyao: [8] Husema, “Anamtegemea BWANA, basi BWANA na amwokoe. Amkomboe basi, kwa maana anapendezwa naye.” [9] Hata hivyo ulinitoa tumboni, ukanifanya nikutegemee, hata nilipokuwa ninanyonya matiti ya mama yangu. [10] Nimekabidhiwa kwako tangu kuzaliwa, toka tumboni mwa mama yangu umekuwa Mungu wangu. [11] Usiwe mbali nami, kwa maana shida iko karibu na hakuna wa kunisaidia. [12] Mafahali wengi wamenizunguka, mafahali wa Bashani wenye nguvu wamenizingira. [13] Simba wangurumao wanaorarua mawindo yao hupanua vinywa vyao dhidi yangu. [14] Nimemiminwa kama maji, mifupa yangu yote imetoka katika viungo vyake. Moyo wangu umegeuka kuwa nta, umeyeyuka ndani yangu. [15] Nguvu zangu zimekauka kama kigae, ulimi wangu umegandamana na kaakaa la kinywa changu, kwa sababu umenilaza katika mavumbi ya kifo. [16] Mbwa wamenizunguka, kundi la watu waovu limenizingira, wametoboa mikono yangu na miguu yangu. [17] Naweza kuhesabu mifupa yangu yote, watu wananikodolea macho na kunisimanga. [18] Wanagawana nguo zangu wao kwa wao, na vazi langu wanalipigia kura. [19] Lakini wewe, Ee BWANA, usiwe mbali. Ee Nguvu yangu, uje haraka unisaidie. [20] Okoa maisha yangu na upanga, uhai wangu wa thamani kutoka nguvu za mbwa. [21] Niokoe kutoka kinywani mwa simba, niokoe kutoka pembe za mafahali mwitu. [22] Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu, katika kusanyiko nitakusifu wewe. [23] Ninyi ambao mnamcha BWANA, msifuni! Ninyi nyote wazao wote wa Yakobo, mheshimuni yeye! Mcheni yeye, ninyi wazao wote wa Israeli! [24] Kwa maana hakupuuza wala kudharau mateso ya aliyeonewa; hakumficha uso wake bali alisikiliza kilio chake ili amsaidie. [25] Kwako wewe hutoka kiini cha sifa zangu katika kusanyiko kubwa, nitatimiza nadhiri zangu mbele ya wale wakuchao wewe. [26] Maskini watakula na kushiba, wale wamtafutao BWANA watamsifu: mioyo yenu na iishi milele! [27] Miisho yote ya dunia itakumbuka na kumgeukia BWANA, nazo jamaa zote za mataifa watasujudu mbele zake, [28] kwa maana ufalme ni wa BWANA naye hutawala juu ya mataifa. [29] Matajiri wote wa dunia watasherehekea na kuabudu. Wote waendao mavumbini watapiga magoti mbele yake, wote ambao hawawezi kudumisha uhai wao. [30] Wazao wa baadaye watamtumikia yeye; vizazi vijavyo vitajulishwa habari za Bwana. [31] Watatangaza haki yake kwa watu ambao hawajazaliwa bado, kwa maana yeye ametenda hili.
