[1] Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu, anga zahubiri kazi ya mikono yake. [2] Siku baada ya siku zinatoa habari, usiku baada ya usiku zinatangaza maarifa. [3] Hakuna msemo wala lugha, ambapo sauti zao hazisikiki. [4] Sauti yao imeenea duniani pote, nayo maneno yao yameenea hadi miisho ya ulimwengu. Katika mbingu amepiga hema kwa ajili ya jua, [5] linafanana na bwana arusi akitoka chumbani mwake, kama shujaa afurahiavyo kukamilisha kushindana kwake. [6] Huchomoza upande mmoja wa mbingu, na kufanya mzunguko wake hadi upande mwingine. Hakuna kilichojificha joto lake. [7] Sheria ya BWANA ni kamilifu, ikihuisha nafsi. Shuhuda za BWANA ni za kuaminika, zikimpa mjinga hekima. [8] Maagizo ya BWANA ni kamili, nayo hufurahisha moyo. Amri za BWANA huangaza, zatia nuru machoni. [9] Kumcha BWANA ni utakatifu, nako kwadumu milele. Amri za BWANA ni za hakika, nazo zina haki. [10] Ni za thamani kuliko dhahabu, kuliko dhahabu iliyo safi sana, ni tamu kuliko asali, kuliko asali kutoka kwenye sega. [11] Kwa hizo mtumishi wako anaonywa, katika kuzishika kuna thawabu kubwa. [12] Ni nani awezaye kutambua makosa yake? Nisamehe makosa yangu nisiyoyajua. [13] Mlinde mtumishi wako na dhambi za makusudi, nazo zisinitawale. Ndipo nitakapokuwa sina lawama, wala sitakuwa na hatia ya kosa kubwa. [14] Maneno ya kinywa changu na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA, Mwamba wangu na Mkombozi wangu.